MWENYEKITI wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, Crescentius Magori amesema ukiacha kitendo cha kufuruhishwa na namna wachezaji wa timu hiyo walivyopambana na kuichapa Yanga jana, lakini mechi hiyo imewaonyesha bado kuna nafasi ya kwenda kuimarisha zaidi kikosi hicho.
Magori amesema tukio la kuumia winga wao Anicet Oura ambaye alicheza mechi hiyo kwa dakika 26 kisha kuingia Seleman Mwalimu, ni tukio ambalo limewapa hesabu hizo kubwa kwa kutafuta watu wengine bora zaidi ili kujenga kikosi kipana.
Mapema tu Oura alionyesha kupata shida kuanzia dakika ya tatu ya mchezo huo wa fainali ya Kombe la Muungano, akishika paja, akajaribu kuendelea kucheza lakini akashindwa kuendelea na kutolewa dakika ya 26.
Simba jana iliipacha Yanga kwa bao 1-0 katika fainali ya Kombe la Muungano iliyochezwa Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.
Akizungumza na Mwanaspoti, Magori amesema: “Tumeupokea kwa furaha sana ubingwa huu, ni moja ya hatua muhimu ingawa bado tuna nafasi ya kufanya vizuri zaidi huko mbele kama tukiendelea kuimarika kama hivi.
“Bahati mbaya mliona Oura aliumia mapema sana, nikajiuliza hapa ataingia nani kocha akamuingiza Mwalimu, lakini ukweli ni tunatakiwa kuendelea kuimarisha timu yetu.
“Tutakwenda kufanya kazi hiyo hapo mbele tutasajili wachezaji bora zaidi ili msimu ujao tuwe na kikosi kipana zaidi kama akitoka Oura basi kuna mashine nyingine inaingia ili tuweze kuwa na ubora uleule.”
Aidha Magori akizungumzia mchezo ujao dhidi ya Yanga, amesema wana hofu kwamba kutakuwa na uchovu mkubwa kwa wachezaji wao kutokana na namna walivyotumika kwenye fainali ya jana.
“Tunataka kwenda kushinda pia lakini naangalia namna ambavyo wachezaji wametumika kwenye mechi hii tunahitaji kufanya kazi kubwa sana ya kuwarudisha kwenye ubora.
“Hii ilikuwa mechi kubwa sana wachezaji wametumia sana nguvu lakini mchezo ujao tena hautakuwa tofauti na huu, unaona Oura amepata maumivu sijajua wengine tutajua zaidi baadaye hali ya wachezaji na kipi kifanyike,” amesema Magori.
Jumapili hii, Simba itakuwa mwenyeji wa Yanga katika mechi ya Ligi Kuu Bara iliyopangwa kuchezwa Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar ikiwa ni raundi ya 20 ya ligi hiyo.
Simba itaingia uwanjani ikiwa imeachwa pointi tano na Yanga inayoongoza msimamo wa Ligi Kuu Bara na imekusanya pointi 47, Simba inazo 42, zote zikicheza mechi 19. Bado mechi 11 kuhitimisha msimu huu.