Home Habari za michezo MASTAA YANGA WAFICHWA ZANZIBAR, SABABU YATAJWA

MASTAA YANGA WAFICHWA ZANZIBAR, SABABU YATAJWA

0

SIKU moja baada ya kikosi cha Yanga kukubali kichapo cha bao 1-0 kutoka kwa watani zao wa jadi, Simba katika fainali ya Kombe la Muungano iliyochezwa Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar, kuna uamuzi mgumu umefanyika kwa mastaa wa timu hiyo, huku sababu ya kufanya hivyo ikitajwa.

Yanga ambayo imevuliwa ubingwa wa Kombe la Muungano kutokana na kichapo hicho ilichopokea Aprili 29, 2026, inakabiliwa na upinzani mwingine kutoka kwa Simba katika mechi ya Ligi Kuu Bara itakayochezwa Jumapili wiki hii kwenye Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam.

Taarifa kutoka kwa kiongozi mmoja wa Yanga, zinasema kwamba, kikosi cha timu hiyo kimesalia Zanzibar kikiendelea na maandalizi ya mechi hiyo ya Jumapili.

Kiongozi huyo aliliambia Mwanaspoti, uamuzi huo umefanyika ili kuweka utulivu ndani ya kikosi baada ya kupoteza dabi ya kwanza kwani hawataki ijirudie kwenye ligi.

“Timu itaendelea kuwepo Zanzibar na tunatarajia kwenda Dar siku ya mechi, tumeamua kufanya hivyo ili kuweka utulivu kwenye timu huku hesabu zikiwa ni kushinda mechi ya Jumapili na kuendelea kujitanua kileleni mwa msimamo wa ligi,” amesema bosi huyo.

Yanga inaongoza msimamo wa Ligi Kuu Bara ikiwa na pointi 47 ikiiacha Simba nafasi ya pili na pointi 42, huku timu zote zikicheza mechi 19.

Dabi hiyo ya Jumapili kila upande inaitazama kwa jicho la karibu zaidi kwani ushindi utabadili hali ilivyo kwenye msimamo.

Wakati hali ikiwa hivyo Yanga, mabosi wa Simba wao wamefanya uamuzi wa haraka kuiwahisha timu Dar es Salaam ili kufanya maandalizi ya mechi ya Jumapili ambayo watakuwa wenyeji.

Katika uamuzi huo, mara tu baada ya mechi ya fainali ya Kombe la Muungano kumalizika sambamba na sherehe zote za kukabidhiwa kombe kufanyika, baadhi ya wachezaji na viongozi wa benchi la ufundi la timu hiyo walirejea Dar fasta kwa usafiri wa ndege, huku wengine wakirejea na boti.

Taarifa ambazo Mwanaspoti ilizipata kutoka Simba, wameamua kufanya hivyo ili kupata muda mzuri zaidi wa kujiandaa kwani bado wana uhitaji wa kushinda mechi hiyo nyingine.

“Wachezaji ambao walianza katika mechi dhidi ya Yanga, waliondoka mapema kwa ndege kurejea Dar es Salaam wakiwa na baadhi ya viongozi wa benchi la ufundi, kisha wale ambao hawakupata muda mwingi wa kucheza au ambao hawakucheza kabisa, walirejea na boti wakiwa na kombe.

“Tumefanya hivyo ili kuwawahisha wachezaji kuja kupumzika, kisha kuanza mara moja maandalizi ya mechi ya Jumapili ambayo pia bado tunahitaji ushindi,” amesema kiongozi mmoja wa Simba.