Home Habari za michezo FADLU KWENYE VITA YA UBINGWA MOROCCO

FADLU KWENYE VITA YA UBINGWA MOROCCO

0

UNAMKUMBUKA Kocha Fadlu Davids aliyekuwa anaiongoza Simba msimu uliopita? Jamaa yuko kwenye vita nyingine kubwa na ngumu ya ubingwa kule Morocco akichuana na kocha mwingine aliyewahi kupita kwa wekundu hao.

Fadlu anayeifundisha Raja Athletic anapigana vita ngumu ya ubingwa na Waarabu hao akipambana na Pablo Franco Martin ambaye naye aliwahi kupita Simba msimu wa 2021/22 wawili hao wakiwania taji la Botola Pro nchini humo akiifundisha Maghreb Fez.

RAJA PRESHA JUU

Kama kuna kitakachonusuru ajira ya kocha huyo basi ni kutwaa ubingwa msimu huu kwani Waarabu hawatakuwa na msamaha naye na watamtimua.

Fadlu alianza kuiongoza Raja Septemba 28, akianzia ugenini dhidi ya Difaa Al Jadid kwa ushindi wa mabao 2-0, Waarabu hao wakishusha presha wakiamini kocha huyo anaweza kuwa mtu sahihi.

Kumbuka msimu wa 2023/24 alikuwa Raja lakini kama msaidizi wa Josef Zinnbauer raia wa Ujerumani na kubeba ubingwa huo na walikuwa wakimbizana vikali na Kocha Nasreddine Nabi aliyekuwa akiifundisha AS FAR Rabat.

Msimu huo ulipomalizika Fadlu alijiunga na Simba msimu uliopita na alijenga timu imara iliyokimbizana na Yanga kusaka ubingwa wa Ligi Kuu Bara na mechi ya mwishoi ndiyo iliyoamua huku Mzauzi huyo akiambulia patupu akipoteza kwa mabao 2-0.

Akiwa Simba alikabiliana na makocha watatu tofauti wa Yanga akianza na Miguel Gamondi, , kisha Sead Ramovic aliyedumu kwa miezi michache na kutimkia CR Belouizdad ya Algeria na Hamdi Miloud aliyemalizia msimu huo.

Simba ilimaliza msimu huo nafasi ya pili na pointi 78, huku Yanga iliyotwaa bingwa ikimaliza na 82, zote zikicheza jumla ya mechi 30, zikipoteza mbili kila moja, lakini Simba iliangushwa na sare nyingi (tatu), huku Yanga ikipata moja.

PABLO NAYE ILIKUWA HIVI

Pablo hakutofautiana safari yake na Fadlu na msimu alioifundisha Simba alimaliza nafasi ya pili na pointi 61, huku Yanga chini ya Kocha Nabi ikitwaa ubingwa na pointi 74 na Mhispaniola huyo aliwaacha Simba njiani baada ya kusitisha mkataba wake.

FADLU MBABE

Msimu huu Fadlu amekutana mara mbili na Pablo Morocco na mechi ya kwanza Msauz huyo akiwa nyumbani alilazimishwa sare ya bao 1-1 lakini alipokwenda ugenini Mei 5, 2026 akashinda kibabe kwa mabao 2-0.

FADLU JUU YA MSIMAMO

Ushindi huo uliifanya Raja kuongoza msimamo wa ligi hiyo ikifikisha pointi 39, huku Maghreb ikiwa nafasi ya pili na pointi 38, zote zikiwa zimeshacheza mechi 19.

Fadlu hadi sasa amepoteza mechi mbili wakati Pablo akiwa amepoteza moja tu lakini Raja iko juu ikinufaika na sare chache ikitoa sita na Maghreb ikiwa na nane .

Pablo katika mechi hizo 19, ameshinda 10, sare nane akipoteza mmoja pekee dhidi ya Raja 2-0 , Maghreb ikiwa imefunga jumla ya mabao 28 wakati ikiruhusu mabao 10, kocha huyo akiing’arisha zaidi timu hiyo kwenye historia ya soka la Morocco.

Fadlu ambaye ambaye alianzia njiani na Raja ameiongoza timu hiyo kwenye mechi 17, akishinda 10 kama ilivyokuwa kwa Pablo, akipoteza mbili na sare sita, vinara hao wakifunga jumla ya mabao 23 na kuruhusu sita.

MOJA KUAMUA

Ubingwa wa msimu huu nchini humo utaamuliwa kwenye mechi ya mwisho iliyosalia kwa kila timu na Raja itakuwa na kibarua nyumbani dhidi ya Wydad Athletic Mei 9,2026, kumbuka dabi hiyo itachezwa bila mashabiki kutokana na vurugu za mashabiki wa timu zote mbili.

Maghreb yenyewe mechi yake ya mwisho itachezwa Mei 10,2026 ugenini dhidi ya Union Touarga ambayo ipo kwenye hatua ya kushuka daraja, ikiwa na kumbukumbu ya kupoteza mechi ya kwanza.

MTIHANI MWISHO WA LIGI

Fadlu atasubiri hadi mechi hiyo ya mwisho kujua hatma yake na ushindi ndiyo utakaoamua abaki na endapo atapoteza lolote linaweza kutokea kwani Waarabu hawana uvumilivu.

Tusubiri kuona kocha gani wa zamani wa wekundu hao atachukua ubingwa msimu huu nchini humo.