Habari za michezo

SHIKANGWA MISIMU MINNE, MABAO 60

Vardo May 11, 2026 11:30 am

MSHAMBULIAJI wa Simba Queens, Jentrix Shikangwa ameendelea kuandika historia ya kipekee baada ya kufikisha jumla ya mabao 60 ndani ya misimu minne, takwimu zinazoendelea kumuweka kwenye orodha ya wachezaji hatari zaidi katika Ligi Kuu ya Wanawake.

Nyota huyo raia wa Kenya alijiunga na Simba msimu wa 2022/23 akitokea Vihiga Queens ya nchini kwao alipokuwa na msimu bora.

Msimu wake wa kwanza, Shikangwa alianza kwa kasi kubwa akifunga mabao 17 katika mechi 13 na kuibuka mfungaji bora wa ligi hiyo inayozidi kukua kwa kasi.

Msimu uliofuata wa 2023/24, alifunga mabao manane katika mechi tisa na aliukosa  mzunguko wa kwanza baada ya Simba kumtoa kwa mkopo kwenda Beijing, China.

Baada ya kurejea, aliendeleza ubora katika msimu wa 2024/25  na alifunga mabao 23 katika mechi 18 akimaliza nafasi ya pili kwa wafungaji bora mbele ya Stumai Abdallah wa JKT Queens aliyemaliza msimu na mabao 27.

Msimu huu hadi sasa mzunguko wa 15, tayari mshambuliaji huyo amefunga mabao 12 akiwa nafasi ya pili kwenye mbio za kusaka kiatu hicho na Jeaninne Mukandayisenga wa Yanga Princess anaongoza kwa mabao 19.

Takwimu hizo zinamfanya Shikangwa kuwa miongoni mwa washambuliaji wenye uwiano mzuri wa mabao kwa kila mechi.

Lakini je, ni nini siri ya muendelezo wa kiwango chake? Hapa anajibu;

“Kwanza namshukuru Mungu. Mimi ni mtu ninayefanya kitu kwa juhudi ambazo zimenifikisha hapa pamoja na kusikiliza kile tunachoambiwa na makocha.”

MALAIKA MEENA AWEKA REKODI ENGLAND HANS FLICK AIPA UBINGWA BARCA SAA CHACHE BAADA YA KUFIWA