SIMBA WATAMBA, SAA NANE MCHANA SIO TATIZO
UONGOZI wa Simba SC umesema haujapatiwa presha yoyote na ratiba ya mchezo wao wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Mbeya City utakaochezwa saa 8:00 mchana katika Uwanja wa Sokoine, Mbeya.
Bodi ya Ligi Tanzania hivi karibuni ilitangaza ratiba ya michezo iliyosalia ya ligi, huku Simba ikipangwa kucheza ugenini dhidi ya Mbeya City Juni 18, 2026 katika muda huo ambao mara nyingi huibua mjadala kutokana na hali ya hewa.
Akizungumzia suala hilo, Meneja wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally, amesema klabu hiyo haina wasiwasi wowote kuhusu muda waliopangiwa kucheza na inaamini mazingira yatakuwa rafiki kwa mchezo huo.
Ahmed alisema kwa kipindi hiki cha mwaka hali ya hewa imekuwa nzuri, jambo linalowapa matumaini ya kucheza bila changamoto kubwa ya joto kali ambalo lingeweza kuathiri kiwango cha mchezo.
“Saa nane mchana kwa sasa ni muda mzuri wa kucheza kutokana na hali ya hewa ilivyo. Hatuna mashaka kabisa na muda huo, na tunaamini timu itafanya vizuri kama ilivyo katika michezo mingine,” alisema Ahmed.
Wakati huo huo, amesema kikosi cha Simba tayari kimerejea mazoezini kuanza maandalizi ya michezo iliyobaki ya Ligi Kuu, huku benchi la ufundi likiendelea kuwanoa wachezaji kwa lengo la kumaliza msimu kwa mafanikio.
Ameongeza kuwa wachezaji ambao hawapo kwenye majukumu ya timu zao za taifa wameendelea na programu ya mazoezi, huku maandalizi yakianza rasmi kuelekea mchezo ujao dhidi ya Pamba Jiji FC kabla ya safari ya Mbeya kuwavaa Mbeya City.