Habari za michezo

Kukosa Penalti Janga Kombe La Dunia

Vardo July 11, 2026 11:29 am

MIAMI, MAREKANI: HAIJALISHI kama Ufaransa wataishia kutwaa au kutotwaa taji lao la tatu la Kombe la Dunia, wengi hawatakumbuka penalti aliyokosa Kylian Mbappe katika ushindi wa robo fainali dhidi ya Morocco.

Mchezo uliochezwa mjini Foxborough ulikuwa bado 0-0 pale Mbappe alipochezewa madhambi na Noussair Mazraoui ndani ya eneo la hatari. Nahodha huyo wa Ufaransa alitumia mbinu ya kusuasua wakati wa kukimbilia mpira kabla ya kupiga penalti, akamtazama kipa Yassine Bounou, lakini shuti lake dhaifu likaokolewa kirahisi.

Hata hivyo, Mbappe alijirekebisha dakika ya 60 baada ya kufunga bao la kuvutia kwa shuti la kupinda lililovunja ukuta mgumu wa Morocco, kabla ya Ousmane Dembele kuongeza la pili dakika sita baadaye na kuipa Ufaransa ushindi wa mabao 2-0.

Pamoja na kuibuka shujaa, kosa lake la awali limezua mjadala mpya: Je, umefika wakati wachezaji waache kutumia mbinu ya kusuasua wanapopiga penalti?

Kwa wapenzi wa soka la zamani, mbinu hiyo imekuwa moja ya mambo yasiyopendwa katika mchezo wa kisasa, sambamba na matumizi ya VAR, wachezaji kuvaa glovu huku wamevaa jezi za mikono mifupi na tabia ya kujiangusha.

Kwa mujibu wa sheria za FIFA, mchezaji anaruhusiwa kupunguza mwendo au kufanya hila wakati wa kukimbilia mpira, lakini haruhusiwi kusimama au kufanya udanganyifu mara tu kabla ya kuupiga.

Mbinu hiyo si ngeni. Mastaa kama John Aldridge, Hugo Sanchez na Pele waliwahi kuitumia kupata faida dhidi ya makipa. Hata hivyo, inaweza kugeuka hasara ikiwa kipa hataamua kujirusha mapema.

Mbappe sasa amejiunga na Bruno Guimaraes, Jorgen Strand Larsen, Lionel Messi na Harry Kane katika orodha ya wachezaji waliokosa penalti baada ya kutumia mbinu ya kusuasua. Kane, hata hivyo, alirudia penalti yake dhidi ya Croatia na kufunga baada ya kuacha kutumia mbinu hiyo.
Takwimu zinaonyesha mbinu hiyo haifanyi kazi sana

Katika Kombe hili la Dunia, penalti 26 zilipigwa kwa kutumia mbinu ya kusuasua, zikiwemo za mikwaju ya penalti. Kati ya hizo, 11 hazikuzaa mabao, ikiwa ni mafanikio ya asilimia 57 pekee.

Mchambuzi wa ITV, Ian Wright amesema: “penalti za aina hii zinaonekana zimeanza kusomwa na makipa. Sasa wanaonekana kuwa mbele ya wapigaji.”

Hata hivyo, wapo waliotumia mbinu hiyo kwa mafanikio, akiwemo Marko Arnautovic, Raul Jimenez, Neymar, Mbappe, Cristiano Ronaldo, Yoane Wissa na Kai Havertz.

Kwa upande mwingine, kati ya penalti 35 zilizopigwa bila kusuasua, 24 zilifungwa, kiwango cha mafanikio cha asilimia 68.

Makipa wamekuwa na nguvu zaidi

Kwa ujumla, Kombe hili la Dunia limekuwa gumu kwa wapigaji wa penalti.

Asilimia 30 ya penalti zilizopigwa ndani ya dakika 90 zimekosa shabaha, ikiwa ni rekodi ya pili mbaya zaidi tangu mwaka 1966. Takwimu zikijumuisha mikwaju ya penalti ya kuamua mshindi, kiwango cha kukosa kinafikia asilimia 35, rekodi mbaya zaidi katika historia ya Kombe la Dunia tangu takwimu zilipoanza kuhifadhiwa.

Mchezaji wa zamani wa Scotland, Pat Nevin amesema: “Kuna vita ya mbinu kati ya wapigaji na makipa. Kufunga penalti siku hizi ni kazi ngumu zaidi kwa sababu makipa wamekuwa warefu, wenye nguvu na wenye kasi.”

Aliongeza: “Kama kipa ataenda upande sahihi, lazima upige shuti kali kabisa pembeni mwa nyavu na hata hivyo bado anaweza kuokoa. Ndiyo maana wapigaji wanatumia mbinu ya kusuasua ili kumdanganya kipa aende upande usio sahihi.”

Nevin pia alieleza makipa wa kisasa wanatumia takwimu nyingi kuwachambua wapigaji. “Hakuna tena siri. Makipa wanajua tabia za kila mpigaji, hivyo kila upande unatafuta mbinu mpya ya kupata faida.”

VAR ilimvuruga Mbappe?

Hii ilikuwa mara ya pili pekee kwa Mbappe kukosa penalti akiwa na Ufaransa, baada ya kufunga 14 kati ya 16 alizopiga. Katika ngazi ya klabu, amefunga 50 kati ya 62.

Lakini mbele yake alisimama Bounou, mmoja wa makipa bora zaidi kwenye penatti. Kipa huyo wa Morocco ameruhusu mabao mawili tu kati ya penalti tisa alizokabili kwenye Kombe la Dunia, huku akiokoa nne na nyingine tatu zikikosa lango.

Mbappe pia anaonekana kuathiriwa na kusubiri kwa muda mrefu kabla ya kupiga penalti yake. Kutokana na uhakiki wa VAR, ilichukua dakika tatu na sekunde 12 tangu itolewe hadi alipopiga na kuokolewa.

Mwandishi wa habari za soka wa Ufaransa, Julien Laurens amesema tatizo kubwa lilikuwa kuvurugika kwa utaratibu wa kawaida wa Mbappe.

“Ilikuwa penati dhaifu na rahisi kwa Bounou kuokoa. Yeye ndiye kipa bora kwenye penati. Taratibu za kawaida ni muhimu sana kwa mchezaji, na safari hii Mbappe alivurugwa kabisa.”

‘Play Off’ Polisi TZ Katika Njia Za Ihefu Na Mashujaa? Prisons Ni Heshima Tu Mngqithi Atamka Makubwa Yanga, Aitaka CAF Champions League