Home Uncategorized SAMATTA KUTUA LIGI KUU ENGLAND AMEACHA DENI KUBWA

SAMATTA KUTUA LIGI KUU ENGLAND AMEACHA DENI KUBWA

NAHODHA wa Taifa Stars, Mbwana Samatta, ni mchezaji halali wa Aston Villa inayoshiriki Ligi Kuu England na tayari ameanza kazi kwenye kikosi hicho.
 Aston Villa hivi sasa inajiandaa kucheza dhidi ya Manchester City katika mchezo wa Fainali wa Kombe la Carabao, na jumamosi itacheza mchezo wa Ligi Kuu England dhidi ya Bournemouth.
 Ni hatua kubwa imepigwa na Samatta katika maisha yake ya soka kwani ameweka rekodi ya kuwa Mtanzania wa kwanza kucheza ligi hiyo ambayo wachezaji wengi duniani wamekuwa wakiwa na ndoto ya kucheza hapo.

Samatta alikuwa na ndoto ya kucheza hapo, ndoto zake zimetimia na sasa jukumu lililobaki ni kuweka rekodi zaidi na zaidi ikiwemo kucheza timu kubwa zaidi ya Aston Villa.
 Haikuwa kazi nyepesi ya kulala na kuamka kisha Samatta kutua Aston Villa, alijitoa, akapambana kufanikisha hili ambalo limetokea kwa sasa.
 Kufika hapo kwa Samatta, ni deni kwa wachezaji wengine wa Kitanzania nao kufuata nyayo zake ili kuwa na namba kubwa ya wachezaji wetu wakicheza ligi kubwa Ulaya.
 Ya Samatta yamepita, lakini yabaki vichwani mwa Watanzania wengi hasa wachezaji soka kwamba na wao wana deni, wanapaswa kulilipa.
 Katika hatua nyingine, tumeona makundi yamepangwa ya mechi za kufuzu Kombe la Dunia michuano inayotarajiwa kufanyika Qatar mwaka 2022.
 Tanzania imepangwa Kundi J na timu za DR Congo, Benin na Madagascar. Ukiangilia kwa haraka unaweza kusema ni kundi jepesi, lakini ni gumu hasa kwetu.
 Mwaka jana tulishiriki Kombe la Mataifa Afrika (Afcon) kule Misri, na timu tulizopangwa nazo zenyewe zilishiriki michuano hiyo ambapo sisi tuliishia hatua ya makundi tukishika nafasi ya mwisho.
 Kundi letu katika Afcon tulikuwa chini ya Senegal, Algeria na Kenya, hatukuweza kushinda hata mchezo mmoja. Kwa ufupi, tulifanya vibaya.
 DR Congo, Benin na Madagascar zilifanya vizuri zaidi yetu. DR Congo iliishia 16 bora, Madagascar wakafika robo fainali kama ilivyo kwa Benin.
 Madagascar ambao waliingia Afcon kama timu isiyopewa nafasi, iliiondosha DR Congo na kuingia robo fainali, huko ikakutana na Tunisia, safari yao ikaishia hapo.
 Benin wao robo fainali walifungwa na Senegal, timu ambayo tulicheza nayo hatua ya makundi na kutufunga.
 Kocha wa Taifa Stars, Etienne Ndayiragije, anapaswa kulitambua hili kwamba, Watanzania wanahitaji kuiona timu ikifanya vizuri na ikiwezekana inakwenda Qatar kushiriki michuano hiyo.
 Hatuwezi kufika Qatar kama hatutakuwa na mipango madhubuti, lazima tukubali tupo kwenye kundi gumu, tukikubali tumepangwa kundi jepesi, itakuwa hatari zaidi kwetu.
 Kukubali kwamba sisi ndiyo timu ya kiwango cha chini kwenye kundi hilo haimaanishi kwamba hatuwezi kupambana, hiyo itawafanya wachezaji kupambana zaidi, matokeo yake tutafikia malengo.
 Dua na sala za Watanzania hivi sasa ni kuona tunashiriki Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi hii.
 Tukiwa tumeshiriki Afcon mara mbili, basi tuna deni la kushiriki Kombe la Dunia. Mikakati iwekwe kufikia malengo hayo.

SOMA NA HII  HAPA NDIPO YANGA ILIPOIPOTEZA SIMBA JUMLAJUMLA