Home Uncategorized NYOTA WATATU WA SIMBA KUIKOSA TANZANIA PRISONS

NYOTA WATATU WA SIMBA KUIKOSA TANZANIA PRISONS


NYOTA watatu wa kikosi cha Simba kinachonolewa na Kocha Mkuu, Sven Vandenbroeck raia wa Ubelgiji akiwa na msaidizi mzawa, Seleman Matola wanatarajiwa kuukosa mchezo wa ligi dhidi ya Tanzania Prisons utakaochezwa Oktoba 22.


Mchezo huo utapigwa Uwanja wa Nelson Mandela, Rukwa saa 10:00 jioni kwa saa za Afrika Mashariki ambapo nyota hao ni pamoja na :-

 Meddie Kagere ambaye ni mshambuliaji namba moja ndani ya kikosi cha Simba akiwa amefunga mabao manne kwa msimu wa 2020/21 anatarajiwa kuukosa mchezo wa Oktoba 22 dhidi ya Tanzania Prisons.


Kagere alipata majeraha kwenye mchezo dhidi ya JKT Tanzania uliochezwa Uwanja wa Jamhuri, Dodoma wakati Simba ikishinda kwa mabao 4-0 huku yeye akifunga mabao mawili kwenye mchezo huo.


Mwingine ni Gerson Fraga, kiungo mkabaji maarufu kama mkata umeme ambaye yeye aliumia kwenye mchezo dhidi ya Biashara United uliochezwa Uwanja wa Mkapa wakati Simba ikishinda kwa mabao 4-0.


Pia nahodha, John Bocco mwenye rekodi ya kufunga mabao zaidi ya 100 ndani ya Ligi Kuu Bara pia anasumbuliwa na majeraha aliyopata kwenye mchezo dhidi ya Mtibwa Sugar.


Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara amesema kuwa wachezaji wote hao watatu kwa sasa wapo kwenye uangalizi wa jopo la madaktari huku wakitegemea maombi ya wanachama na mashabiki wa Simba kuwaombea dua njema nyota hao ili warejee kwenye ubora wao.


Simba ipo nafasi ya pili kwenye msimamo ikiwa na pointi 13 baada ya kucheza mechi tano inakutana na Tanzania Prisons iliyo nafasi ya 13 na pointi zake sita baada ya kucheza mechi sita.

SOMA NA HII  KUMBE ILE SARE YA MABAO 3-3 YA YANGA NA SIMBA, SIMBA WALILIA DAKIKA 15