Home Uncategorized NYOTA BURUNDI AIPA TANO YANGA USAJILI WA NTIBAZONKIZA

NYOTA BURUNDI AIPA TANO YANGA USAJILI WA NTIBAZONKIZA


 BIGIRIMANA Blaise, mshambuliaji namba moja ndani ya Klabu ya Namungo amesema kuwa usajili wa Yanga kwa nyota Said Ntibazonkiza ni mzuri kwa kuwa wamepata mashine ya kazi.

 Ntibazonkiza alisajiliwa na Yanga Oktoba 12 anacheza pamoja na Blaise anayecheza ndani ya Klabu ya Namungo kwenye timu ya Taifa ya Burundi ambayo inasaka tiketi ya kuwania kufuzu Afcon itakayofanyika nchini Cameroon 2022.


Akizungumza na Saleh Jembe, Blaise amesema kuwa nyota huyo hana uwezo wa kukata tamaa ndani ya uwanja jambo ambalo linamfanya anakuwa bora muda wote.


“Kuhusu mshambuliaji mpya wa Yanga ambaye tunacheza naye timu ya Taifa ya Burundi ni balaa tupu analoonyesha uwanjani, hajui suala la kukata tamaa yeye anapambana kusaka matokeo katika hilo waliomsajili hawajakosea.


“Matumaini yangu ni kwamba atafanya mengi mazuri ikiwa atapewa nafasi kwa kuwa yupo vizuri na ninamtambua hataweza kuwaangusha,” amesema.

Nyota huyo kwenye timu ya Taifa ya Burundi amefunga jumla ya mabao manne kwenye mechi za hivi karibuni alifunga bao moja mbele ya Tanzania, Oktoba 11 mchezo wa kirafiki na mabao matatu aliwafunga Mauritania, mchezo wa kwanza Novemba 11 alifunga bao moja na mchezo wa pili Novemba 15 alifunga mabao mawili katika kuwania tiketi ya kufuzu Afcon.

Anatarajiwa kutua Bongo Desemba 15 baada ya dirisha dogo la usajili kufunguliwa ndani ya ardhi ya Tanzania.

SOMA NA HII  SIMBA YAIWEKA KANDO YANGA