Home news KAMA GATOGATO AMEWEZA, KAYOKO NA SASII HAWAWEZI KUSHINDWA

KAMA GATOGATO AMEWEZA, KAYOKO NA SASII HAWAWEZI KUSHINDWA


MICHUANO ya kombe la mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ndani imemalizika Jumapili nchini Cameroon, kwa fainali kali kupigwa kati ya timu ya Taifa ya Morocco dhidi ya Mali.

Michuano ya mwaka huu ambayo imeshirikisha takribani timu 16 zilizowekwa katika makundi manne, imekuwa na ushindani wa aina yake licha ya hapo awali kuahirishwa kutokana na janga la virusi vya Corona ambalo limekuwa tishio kwa maeneo mbalimbali duniani.

Miongoni mwa timu zilizopata nafasi ya kushiriki michuano hiyo kwa mwaka huu ni timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars ambayo ilishiriki michuano hiyo kwa mara ya pili baada ya kufanya hivyo mara ya kwanza mwaka 2009.

Kwa bahati mbaya kama ilivyokuwa mwaka 2009, katika michuano ya mwaka huu pia Stars iliishia katika hatua ya makundi wakiwa wamejikusanyia pointi 3 tu ndani ya kundi C lililokuwa na timu za Zambia, Namibia na Guinea.

Yapo mengi ambayo naamini timu yetu ya Taifa imejifunza kupitia michuano hii, hasa kwa sababu kiasi kikubwa cha nyota wengi walioitwa kwenye kikosi na kocha Ettiene Ndayiragije walikuwa ni wapya.

Lakini miongoni mwa mambo mengi ambayo sisi kama Watanzania tumejifunza kupitia michuano hii ni juu ya ubora wa viwango vya waamuzi waliopata nafasi ya kuchezesha michezo hiyo.

Wengi wetu mtakubaliana na mimi kuwa waamuzi waliochezesha CHAN ya mwaka huu, walifanikiwa kuonyesha uwezo mkubwa wa kutafsiri zile Sheria 17 za mchezo wa soka.

Waamuzi hawa sio Malaika hivyo hata kama walifanya makosa basi ni mara chache sana tena ni yale ambayo tunayataja kuwa makosa ya kibinadamu, lakini pia waamuzi hawa hawajatoka sayari nyingine bali kuna wengine wametoka hapo kwa Wanaafrika Mashariki wenzetu Taifa la Burundi.

Nadhani hapa ndipo tunapopata swali la kuwauliza waamuzi wetu wa Kitanzania, ni nini ambacho wamejifunza kutoka kwa wenzao, na nini wanadhani imekuwa sababu kubwa ya kupelekea kukosekana kwa mwamuzi hata mmoja wa Tanzania ambaye amekwenda kuchezesha michuano hii?

SOMA NA HII  BAADA YA KUKINUKISHA SIMBA...MGHANA WA AZAM AMPA SOMO MORRISON...AFUNGUKA YASIRINI...

Lazima tukubali kuwa bado kuna changamoto ya ubora kwa waamuzi wetu, na hili limekuwa likithibitishwa mara kwa mara na malalamiko mengi ya wadau wa soka hapa nchini, na hata kupitia adhabu zitolewazo na bodi inayosimamia uendeshwaji wa ligi kuu (TPLB).

Na baada ya kukiri tatizo hilo tujiulize tunawezaje kulipunguza kama sio kuliondoa kabisa, kama ni kuendesha kozi za mafunzo, kuboresha mazingira ya kazi, kuongeza vifungu vya adhabu kwa waamuzi watakaokiuka miiko ya kazi zao au hata kuangalia upya mchakato wa kutoa vibali vya kazi kwa waamuzi hao.

Naamini ili kuweza kufika huko tunahitaji kufanya maamuzi tu, na wala haiwezi kuwa kitu kigumu. Kama mwamuzi, Georges Gatogato wa Burundi ameweza kuchaguliwa na CAF kusimama katika michezo ya CHAN, naamini hata waamuzi wetu, Ramadhani Kayoko na Hery Sasii wanaweza.

Uchambuzi wa Lunyamila kupitia gazeti la Championi Jumatatu.