Home Azam FC TP MAZEMBE YAIJAZA AZAM JEURI MBELE YA SIMBA

TP MAZEMBE YAIJAZA AZAM JEURI MBELE YA SIMBA


UWEZO ulioonyeshwa na kikosi cha klabu ya Azam kwenye mchezo wa Kimataifa wa Kirafiki dhidi ya TP Mazembe, umelifanya benchi la ufundi la timu hiyo kuamini sasa wako tayari kwa mchezo wa kiporo cha ligi dhidi ya Simba.


Azam Jumanne ya wiki hii ilionyesha kiwango bora licha ya kulazimishwa sare ya bao 1-1 dhidi ya TP Mazembe katika mchezo wa kimataifa wa kirafiki uliopigwa katika uwanja wa Azam Complex, Chamazi jijini Dar es Salaam.


Azam na Simba zinatarajiwa kuvaana Jumapili hii katika mchezo mkali wa kiporo cha Ligi Kuu Bara.


Akizungumzia maandalizi yao, Mkuu wa Kitengo cha habari na mawasiliano wa klabu ya Azam, Zakaria Thabith ‘Zaka za Kazi’ amesema kikosi hicho kimeanza rasmi kambi ya kujiandaa na mchezo huo jana Alhamisi baada ya likizo ya siku moja.


“Kocha mkuu George Lwandamina ameridhishwa na kiwango ambacho kikosi kimeonyesha katika michezo yote mitano ya kujipima nguvu kwa ajili ya kujiandaa na michezo ya Ligi Kuu Bara.


“Mchezo uliopita dhidi ya Mazembe umempa taswira kamili ya utayari wa wachezaji wake kuelekea mchezo ujao wa ligi dhidi ya Simba.


“Tayari tumeanza rasmi maandalizi ya mchezo wetu dhidi ya Simba, baada ya likizo ya siku moja, ambapo tumejipanga kutumia mchezo huo kurejea tena kwenye ushindani,”

SOMA NA HII  DILI LA SHABANI DJUMA NA AZAM ...MAMPYA YAIBUKA....