Home Yanga SC MUAMBIENI NTIBANZOKIZA, YANGA KUBWA KULIKO BURUNDI

MUAMBIENI NTIBANZOKIZA, YANGA KUBWA KULIKO BURUNDI


Na Saleh Ally

UMEONA baadhi ya wale wanaofanya kazi na Yanga ambao sidhani kama itakuwa sahihi kuwaita viongozi wameshindwa kuona mshambuliaji wao, Saido Ntibanzokinza amekosea na wameungana naye kutengeneza kosa tena la kuficha makosa.

Ajabu, hata baadhi ya mashabiki, nao wakaona sawa na kuanza kumshambulia karibu kila aliyesema Ntibanzokiza amekosea. Hii inaonyesha kiasi gani suala la uelewa wetu katika michezo limefunikwa na jambo furaha au faraja ambayo imekuwa chachu kubwa ya kuziangusha klabu zetu kubwa na zikashindwa kusonga mbele.

Leo, akitokea mtu ana nafasi ya kuifanya Yanga iwe inapata ushindi tu, lakini akawa hapiti njia sahihi kwa maana ya uongozi au utoaji misaada yake, bado atabaki kuwa shujaa kwa kuwa mashabiki wengi wanachoangalia ni ushindi wa uwanjani pekee ambao unaweza kuwa sehemu kubwa ya maendeleo ya muda mfupi na si mrefu na hili limetokea sana.

Ntibanzokiza aliingia akichukua nafasi ya Tuisila Kisinda aliyekuwa ameumia wakati Yanga ikiivaa Gwambina ya Misungwi, Mwanza. Dakika chache baadaye akapokea pasi maridadi kabisa ya Michael Sarpong na kufunga kwa ujuzi mzuri kabisa.

 Hakika lilikuwa bao zuri kabisa lakini ajabu, mara baada ya tu ya kufunga hilo bao akaanza kuomba atolewe.

Lilikuwa bao la tatu kwa Yanga, ni muhimu kwa sababu linaisaidia Yanga kushinda kwa mabao matatu baada ya muda mrefu, maana yake linainua morali. Kile kitendo cha Ntibanzokiza kuomba atolewa huku akishika kichwa chake kuonyesha kwamba ana akili, ikiwa wazi sote tunaona ni ishara kwamba anafikisha ujumbe kwa Kocha Juma Mwambusi aliyemuweka benchi.

Bila ya ubishi, hakuna namna ya kulipindisha jambo hilo. Kwamba Ntibanzokiza hakuwa amesema hivyo au vinginevyo maana tumeona sote wachezaji wengine wakimbembeleza kurudi uwanjani kwa kumsihi na kumsisitiza kwamba si sahihi.

Tumeona sote baadhi ya wachezaji wakipinga na kuonyesha kukerwa na kitendo hicho, dalili inayoonyesha huenda hata mazoezini mambo kama hayo hutokea. Ingekuwa ni mara ya kwanza, wachezaji wengine wasingeokana kukerwa na jambo hilo.

Hivyo, wale ambao wanaona mchezaji mzuri au mahiri au yule anayefunga bao basi anaweza kufanya lolote hata la utovu wa nidhamu bila ya kuguswa au kuhojiwa au kukosolewa, wajue wanakosea sana.

SOMA NA HII  KUELEKEA MECHI YA KESHO...NABI ANGIWA MCHECHETO DHIDI YA NAMUNGO..ADAI NI WAGUMU...

Hauwezi ukaikuza klabu ikawa ni inayofuata weledi, ikawa bora inayofanya vizuri kama ndani yake kutakuwa na wachezaji wakubwa zaidi ya klabu yenyewe.

Wachezaji wanapaswa kuiheshimu klabu kama ‘platform’ inayowafanya wao kuonekana, inayofawanya wao kuonyesha uwezo wao walionao. 

Yanga haijawahi kucheza kwa niaba ya Ntibanzokiza ila Ntibanzokiza ndiye anacheza kwa niaba ya Yanga na anavaa jezi ya Yanga, hivyo anapaswa kuiheshimu.

Hata ukiwa na mtoto wako nyumbani anafaulu sana shule lakini lazima awe na heshima, lazima kuwe kuna usawa wa maisha kwa maana ya nidhamu na mengineyo hata na wale wasiofaulu sana. Si kwamba akifaulu tu, basi anaruhusiwa hata kudharau wengine, haiwezekani na haiwezi kuwa familia bora.

Nimemsikia mkongwe na ‘legend’ wa Yanga, Bakari Malima ‘Jembe Ulaya’ akisisitiza kwamba Ntibanzokiza amekosea na aombe tu radhi. Baadhi wamemshambulia kwa maneno makali, yote haya ni kutojitambua, huu ndio ukweli, Ntibanzokiza hawezi kuwa mkubwa kuliko Yanga na ndiyo maana Yanga ikamuajiri yeye.

 Hivyo mpendeni lakini atambue mipaka yake

kwamba yeye ni mchezaji kama wengine na hana uwezo wa kumpangia kocha kikosi.

Angalia mchezaji kama Meddie Kagere wa Simba, mfungaji bora mfululizo kwa misimu miwili, sasa ndiye aaongoza kwa mabao lakini Simba anawekwa benchi na anasubiri na akipata nafasi anaonyesha juhudi, kwani Ntibanzokiza ameifanyia Yanga mangapi kwa muda gani hadi awe mkubwa hivyo hataki kuwekwa benchi na akiwekwa aonyeshe ujeuri wa kiwango hicho tena mbele ya macho ya Wanayanga maelfu na wapenda michezo wengine mamia kwa maelfu.

Ungeniambia nimkumbushe Ntibanzokiza kuhusiana na Yanga, ningemuambia Yanga ni kubwa kuliko hata nchi yake ya Burundi. Idadi ya watu Burundi haizidi milioni 15 lakini Yanga ina mashabiki zaidi ya milioni 20.Ukubwa huu unapaswa kuheshimiwa.

Mjifunze, kama Ntibanzokiza leo anakosea na apewa sehemu ya kuzungumza kwenye nyenzo za klabu ili azungushe maneno badala ya kuomba radhi, basi mjue madhara yake ni makubwa baadaye kwa kuwa mnawavimbisha vichwa watu, ila mtakuwa mnajenga wigo wa tabia za hovyo.