Home Azam FC ISHU YA UBINGWA VPL… AZAM WAZIONYA SIMBA NA YANGA

ISHU YA UBINGWA VPL… AZAM WAZIONYA SIMBA NA YANGA

 


WAKIWA wamesaliwa na pointi moja pekee kuzifikia Simba na Yanga kwenye vita ya kusaka ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu, Uongozi wa kikosi cha klabu ya Azam umefunguka kuwa, hawana presha yoyote na ubingwa, na kinachotakiwa kwa sasa ni kila mtu ashinde mechi zake.

Azam Alhamisi iliyopita waliibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Biashara United na kufikisha pointi 60 zinazoendelea kuwaweka katika nafasi ya tatu ya msimamo wa Ligi Kuu Bara, wakizidiwa pointi moja pekee na vinara wa msimamo klabu za Simba na Yanga ambao wote wana pointi 61 katika nafasi ya kwanza na ya pili ya msimamo.

Mabingwa hao wa Ligi Kuu Bara msimu wa 2013/14 wako fomu ambapo, katika michezo yao saba iliyopita wamefanikiwa kuibuka na ushindi katika michezo sita na kutoa sare moja, hivyo kujikusanyia pointi 19 kati ya 21 katika michezo hiyo, ambapo mpaka sasa wamesaliwa na michezo minne pekee kumaliza ligi.

Akizungumzia malengo yao nahodha wa Azam, Aggrey Morris amesema: “Tunashukuru Mungu kwa kasi ambayo kikosi chetu inayo kwa sasa, tulipitia kipindi kigumu hapo kabla na kurejea kwenye fomu hii ni jambo la kujivunia sana.

“Tuko katika nafasi ya tatu na tofauti ya pointi moja pekee dhidi ya Simba na Yanga, licha ya wenzetu kuwa na michezo ya viporo lakini niweke wazi kuwa, hatuna presha ya ubingwa kinachotakiwa ni kila mtu ashinde mechi zake halafu maswala ya ubingwa yatakuja baadaye.”

SOMA NA HII  KISA SAFARI YA ZANZIBAR ALLY KAMWE AMPIGA KIJEMBE FEI TOTO