Home Azam FC AZAM FC ILE YA NUSU FAINALI IJITAFUTE MUDA WOTE

AZAM FC ILE YA NUSU FAINALI IJITAFUTE MUDA WOTE


 NUSU fainali katika fainali ya Kombe la Azam Sports Federation kati ya Azam FC dhidi ya Simba ilikuwa ni nusu fainali ndani ya fainali kamili.

Ulipigwa mchezo mkubwa katika Uwanja wa Majimaji licha ya ubora wa uwanja kuwa kikwazo kwa kuwa timu zote mbili wachezaji wake ni wale ambao wamezoea kucheza katika viwanja visivyopenda shida.

Ukianza na Azam FC, Uwanja wa Azam Complex ule wenye nyasi bandia ni pendwa kwao kufanyia mazoezi huku Simba wao wakiwa wanatamba ndani ya Simba Mo Arena kule Bunju.

Weka kando masuala ya uwanja kwa kuwa timu zote zilikuwa pale zikicheza ni wakati wa kutazama namna gani viwanja vyetu tutaweza kuboresha na kuvifanya kuwa bora.

Kuhusu matokeo hakuna ambaye anaweza kuyabadili kwa kuwa mambo yalikuwa ni harakaharaka na Azam FC wenyewe wameweka wazi kwamba wamekubali yaliyotokea kwa kuwa mwenye maamuzi ya mwisho ni mwamuzi.

Lakini kwa waamuzi pia ni muhimu kuweza kusimamia sheria 17 za soka katika maamuzi ili kuweza kutenda haki kwa timu zote bila kujali kwamba ni Simba, Yanga, Njombe Mji ama Kagera Sugar.

Jambo ambalo ninaweza kusema kwamba Azam FC ni moja ya timu bora lakini kuna mechi nyingine inacheza ikiwa chini ya kiwango jambo linalowafanya wapate matokeo ambayo hawajatarajia.

Mchezo wao wa mwisho kwenye ligi nilitazama namna walivyocheza na Namungo pale Uwanja wa Majaliwa mambo yalikuwa tofauti na ile Azam FC ambayo ilianza msimu kwa kasi ya kutimiza jambo.

Labda unaweza kusema kwamba ilikuwa ni suala la Uwanja wa Majaliwa kuwa sio sawa na ule wa Azam Complex bado hata walipokutana kwenye mchezo wa kwanza ngoma ilikuwa nzito.

Weka kando mchezo huo hata walipokutana na Ruvu Shooting ilikuwa ni pira gwaride v pira Ice Cream bado Azam FC ilikuwa kwenye kiwango cha kawaida haimaanishi kwamba nawabeza wapinzani wao hapana.

Weka kando masuala ya waamuzi tunahitaji kuona mwendelezo wa timu zote hapa Bongo ukiwa katika kasi yake ileile daima.

SOMA NA HII  FT:YANGA WAPITA MULEMULE WALIKOPITA SIMBA....WABEBA NDOO NYINGINE KIBABE....

Kwa nini Azam FC inafanya vizuri mwanzo kisha ikifika kati mambo yanakuwa magumu hapa panatakiwa patafutiwe ufumbuzi na wenye Azam yao.

Mashabiki wa Azam FC ni miongoni mwa mashabiki wenye kujitoa kwa ajili ya Azam FC na timu ya Azam FC mafanikio yake ni ramani ya Tanzania kwa kiasi kikubwa kwa kuwa ni chimbuko la wachezaji wote mastaa vizazi vya wakati huu kutokana na kuwa na malezi bora.

Hapo sasa ndipo inakuwa ni pasua kichwa kwa wamiliki kupambana kuifanya Azam kuwa bora wakati wote. Nina imani kwamba ile sera inayotumika na timu hiyo kwenda kukabiliana na Simba ama Yanga itumike muda wote.

Nusu fainali ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Simba ulipigwa mpira wa kiwango, wanaume walikuwa kazini na walifanya kweli, basi wajitafute muda wote wawe kwenye kiwango kile.

Kuna kupanda na kushuka hiyo ipo ila bado kuna tofauti ya kupanda na kushuka kwa Azam FC ni timu ambayo ikishuka morali sehemu ndogo kurejea inaweza kuchukua muda mrefu.

Azam FC ina kila kitu basi ni wakati wake sasa kuendeleza utawala wake wa ubora ndani ya uwanja kama ambavyo imefanikiwa kufanya nje ya uwanja kwa uwekezaji.