Home Yanga SC YANGA YAIWEKA SIMBA KIPORO

YANGA YAIWEKA SIMBA KIPORO


 BAADA ya ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Simba, Julai 3, 2021 Uwanja wa Mkapa, Yanga wamewaweka kando mabingwa hao watetezi kuelekea kwenye mchezo wao wa Kombe la Shirikisho unaotarajiwa kuchezwa Julai 25.

Bao pekee la ushindi la Yanga lilifungwa na Zawadi Mauya dakika ya 12 na kuwapa pointi tatu mazima Yanga inayonolewa na Kocha Mkuu, Nasreddine Nabi.

Ofisa Habari wa Yanga, Hassan Bumbuli amesema kuwa kwa sasa akili zao ni kwenye mechi za ligi kisha watahamishia nguvu kwenye mchezo wao wa fainali wa Kombe la Shirikisho.

“Nguvu kwa sasa tunazipeleka kwenye mechi za ligi kwa kuanza na huu dhidi ya Ihefu kisha na ule dhidi ya Dodoma, tunatambua kwamba itakuwa migumu lakini tunahitaji pointi tatu.

“Kazi hii ikiisha tunageuka kwenye kazi nyingine ila ikumbukwe kwamba tuliweka wazi kwamba tunahitaji kutwaa mataji yote mwaka huu hivyo kuelekea katika fainali tunaamini kwamba tutapata matokeo,” amesema Bumbuli.

Kwenye msimamo Yanga ipo nafasi ya pili baada ya kucheza mechi 32 ina pointi 70 huku Simba ikiwa nafasi ya kwanza na pointi 73.

Katika mchezo wao wa mzunguko wa kwanza walitoshana nguvu kwa kufungana bao 1-1 ila mzunguko wa pili Yanga ilishinda.

Wanatarajiwa kukutana kwenye mchezo wa fainali ya Kombe la Shirikisho ambalo mabingwa watetezi ni Simba hivyo unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa.

Yanga inatarajiwa kucheza na Simba Julai 25 kwenye fainali ya Kombe la Shirikisho, Uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma.

SOMA NA HII  YANGA YAKIRI KUWA MCHEZO WA RIVERS UNITED HAUTAKUWA MWEPESI