Home news YANGA YATIBUA TENA SHUGHULI YA SHEREHE ZA UBINGWA WA SIMBA

YANGA YATIBUA TENA SHUGHULI YA SHEREHE ZA UBINGWA WA SIMBA


 KUELEKEA fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam itakayopigwa Julai 25, mwaka huu kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma, kasi ya Yanga imewashtua Simba ambao wamelazimika kupunguza shamrashamra za ubingwa wao ili kupata muda wa kutosha kujiandaa na mchezo huo.

 

Leo jioni kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar, Simba wanatarajiwa kukabidhiwa kombe lao la Ligi Kuu Bara walilolitwaa msimu huu kwa mara ya nne mfulululizo, baada ya mchezo dhidi ya Namungo.


Akizungumza na Spoti Xtra, kuhusiana na sherehe za ubingwa wao, Meneja wa Simba, Patrick Rweyemamu, alisema: “Kwa sasa tumewekeza mawazo yetu kwenye mchezo dhidi ya Namungo utakaochezwa Jumapili.

 

“Utaratibu wa sherehe za ubingwa utatolewa rasmi na uongozi wa juu, lakini hata hivyo hatutarajii kuwa na sherehe kubwa kwa sababu bado tuna mchezo wa fainali ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Yanga na tunataka kuanza mapema maandalizi ya mchezo huo kwa kuwa malengo yetu ni kutetea kombe hilo.”

 


Msimu uliopita Simba ilikabidhiwa ubingwa wao katika mchezo dhidi ya Namungo uliochezwa mkoani Lindi, ilipotua Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar, kulikuwa na maandalizi ya kusherehekea ubingwa huo kwa kuandaliwa gari la wazi.

 

Sven Vandenbroeck aligomea sherehe hizo akitaka vijana wake waingie kambini kujiandaa kuwakabili Yanga katika mchezo wa nusu fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam uliochezwa Julai 12, mwaka jana Uwanja wa Mkapa, Dar ambapo walifanikiwa kuibuka na ushindi mnono wa mabao 4-1.

Hivyo msimu huu unakuwa wa pili kwa Yanga kutibua shughuli za ubingwa wa Simba ambayo kwa sasa inanolewa na Kocha Mkuu, Didier Gomes.

SOMA NA HII  SAKATA LA KUJIUZULU BARBARA...MENGINE MAPYA YAIBUKA...ALIKUWA HAZIIVI NA 'TRY AGAIN'....