Home news BAADA YA KOCHA MPYA WA VIUONGO KUTAJWA JANA…MBRAZILI AWAPA SIMBA KOCHA WA...

BAADA YA KOCHA MPYA WA VIUONGO KUTAJWA JANA…MBRAZILI AWAPA SIMBA KOCHA WA MAKIPA..

 


WATETEZI wa Ligi Kuu Bara, Simba wanaendelea kulisuka benchi lao la ufundi na siku chache kuanzia sasa watawashusha makocha wengine wawili wapya, huku aliyekuwa kocha wa makipa wa timu hiyo, Milton Nienov akiwapa ramani mabosi wake wa zamani kocha wa aina gani atakayewafaa.

Ilifahamika kuwa kocha wa viungo raia wa Hispania ndio atakuwa wa kwanza kushuka nchini na baada ya hapo atafuata wa makipa ambaye atakuja kuwanoa, Aishi Manula, Benno Kakolanya, Ally Salim na Jeremiah Kisubi.

Katika kuhakikisha wanapata kocha bora wa makipa uongozi wa Simba umemuachia kazi mkuu wa benchi la ufundi, Pablo Franco ataje kocha anayemhitaji katika nafasi hiyo kisha kuangalia uwezekano wa kumpata.

Aliyekuwa kocha wa makipa, Mbrazil Milton Nienov amenukuliwa na gazeti la Mwanaspoti kwamba kikosi cha Simba kina makipa bora ambao hata mfundishaji wao hatakuwa na kazi ngumu.

Milton alisema Simba inahitaji kocha wa makipa mzuri wa kuwaelekeza makipa wake mambo machache katika kuokoa mashambulizi na kusahihisha makosa yao ila maeneo mengine kote wapo vizuri.

“Pengine ndio maana nilifanikiwa kutengeneza ubora wa makipa wangu kwani baada ya kuwapa misingi ya kazi zao wanapokuwa uwanjani nilikuwa naweka nguvu zaidi katika mbinu na kiasi kikubwa wote waliiimarika,” alisema Milton na kuongeza;

“Kama wakimpata kocha wa namna hiyo ambaye ni mzuri katika mbinu na kurekebisha makosa ndio watafanikiwa zaidi lakini wakimpata ambaye si mzuri kwenye maeneo hayo watakuwa na changamoto.”

Wakati Milton akiwa kwenye majukumu ya makocha wa makipa Simba alifanikiwa kuboresha uwezo wa Aishi Manula ambaye alikuwa chaguo la kwanza na kutokufungwa mabao ya mepesi tofauti na ilivyokuwa kabla ya hapo.

Aliyekuwa kocha wa makipa wa Simba, Muharami Mohammed ‘Shilton’ alisema kwa nyakati tofauti huwa anazungumza na makipa watatu wa timu hiyo, Manula, Kakolanya na Salim.

“Kama nikimuona Manula amekosea katika eneo fulani huwa namuelekeza alitakiwa kufanya nini na huenda kufanyia kazi, vivyo hivyo kwa wengine lakini hata wakifanya vizuri huwa nawaeleza pia,” alisema Milton na kuongeza;

SOMA NA HII  KASI YA BENCHIKHA YAWASHITUA MAKOCHA

“Walivyo makipa hao watatu wa Simba kocha ambaye anahitajika hapo ni kuhakikisha ubora wao haupotei ili viwango vyao vilingane hata ikitokea mmoja amekosekana mwingine acheze bila shida.”