Home Azam FC JERAHA LA LYANGA LAZUA HOFU AZAM…AFANYIWA X-RAY…YABAINIKA KAVUNJIKA PUA NA ….

JERAHA LA LYANGA LAZUA HOFU AZAM…AFANYIWA X-RAY…YABAINIKA KAVUNJIKA PUA NA ….


KIUNGO mshambuliaji wa Azam, Ayoub Lyanga, anaendelea vizuri baada ya kutokwa na damu puani wakati wa mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Geita Gold.

Nyota huyo alikutana na kadhia hiyo wakati akiwania mpira kwenye mchezo huo uliofanyika katika Uwanja wa Azam Complex, uliopo Chamazi na wenyeji kuibuka na ushindi wa bao 1-0, lililofungwa na Mzambia Rodgers Kola dakika ya 80.

Daktari Mkuu wa timu hiyo Mwanandi Mwankemwa, alisema kuwa mchezaji huyo alifanyiwa vipimo vya X-Ray katika Hospitali ya Ekenywa iliyopo Magomeni Jijini Dar es Salaam na kugundulika kuvunjika mfupa wa pua pamoja na jino.

“Hali yake inaendelea vizuri kwa sasa maana damu iliyokuwa inatoka kwa wingi haitoki tena hivyo itamchukua muda wa wiki mbili kurejea kwenye hali yake ya kawaida,” alisema.

Mbali na kuvunjika jino ila Mwankemwa aliongeza kuwa Lyanga alipata pia mpasuko juu ya meno yake ambayo yalimsababishia kutokwa na damu kwa wingi.

“Baada ya kuona tatizo hilo ilitubidi kumpeleka kwa madaktari ambao wamebobea kwenye taaluma ya kutibu masikio, pua na koo, ambao tunaamini watamsaidia ili kurejea kwenye hali zuri,” alisema Dk. Mwankemwa.

Lyanga anaungana na mshambuliaji wa timu hiyo Prince Dube ambaye amekuwa nje ya Uwanja tangu alipoumia kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) dhidi ya Rhino Rangers Mei 26, mwaka huu.

SOMA NA HII  KAIZER CHIEFS WAMNYEMELEA MRITHI MA MAYELE YANGA...JAMAA LINATUPIA SIO KITOTO ...