Home news WAKATI WATU WAKIITAJA GSM TU KWENYE MAFANIKO YA YANGA…MANARA AIBUKA NA ‘KUWAZODOA’...

WAKATI WATU WAKIITAJA GSM TU KWENYE MAFANIKO YA YANGA…MANARA AIBUKA NA ‘KUWAZODOA’ KWA HILI…


UONGOZI wa Yanga umewataka mashabiki wa timu hiyo wategemee furaha tu kutokana na uwezo mkubwa wa kikosi walichonacho kinachoweza kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu chini ya uongozi imara na benchi la ufundi bora.

Yanga kwa sasa ndio vinara wa ligi kuu wakiwa na pointi 35 wakiwa wanawapita wapinzani wao Simba kwa pointi 10.

Akizungumza na gazeti la Spoti Xtra, Msemaji wa Yanga, Haji Manara, alisema kwa sasa Wanayanga wawe na furaha kubwa kutokana na uwezo unaooneshwa na wachezaji wa timu hiyo ambao ni wazi wataipatia ubingwa Yanga msimu huu.

“Yanga kwa sasa kwetu ni raha tu, kwanza kuanzia benchi la ufundi kuna watu sahihi, uwezo wa kocha Nabi ni mkubwa sana na uwezo wa wachezaji ni wa hali ya juu, Yanga sio tu kuna wachezaji wengi, lakini tuna kikosi kipana na cha ushindani.

“Kwa sasa ndani ya Yanga kila mchezaji atakayeanza basi ujue kuwa ana uwezo wa kuipatia timu matokeo mazuri ndio maana utaona tumepata ushindi katika mchezo wa Mbao na kikosi tofauti na kile ambacho tulipata ushindi dhidi ya Polisi Tanzania,” alisema kiongozi huyo.

Yanga ambayo ni vinara wa Ligi Kuu Bara, Kocha Mkuu wa Yanga, Nasreddine Nabi, anakuna kichwa ndani ya dakika 360 za moto kusaka ushindi katika mechi nne ambazo zinazotarajiwa kuchezwa ndani ya Februari hii.

Dakika hizo 360, mechi tatu za Ligi Kuu Bara na moja Kombe la Shirikisho la Azam Sports, Yanga itaanza wikiendi hii kupambana na Mbeya City, kisha itamenyana na Biashara United katika hatua ya 16 bora kwenye Kombe la Shirikisho.

Baada ya hapo, Februari 23, itakuwa Uwanja wa Manungu, Morogoro kucheza mechi ya ligi dhidi ya Mtibwa Sugar.

Yanga itamaliza mwezi huu kwa kucheza dhidi ya Kagera Sugar, itakuwa ni Februari 27 kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar, hivyo kukamilisha safari ya dakika 360 za kusaka ushindi.

Nabi aliliambia Spoti Xtra kuwa: “Kazi kubwa iliyopo kwenye mechi zote ni kusaka ushindi bila kujali tunacheza na timu ipi.”

SOMA NA HII  HUYO CHICO KWA MIPASI TU..? NI BALAAH...PABLO AWAPIGA STOP MASTAA SIMBA KULA CHIPSI ZEGE....