Home Habari za michezo HATIMAYE BALEKE ABEBESHWA MIZIGO SIMBA…MSIMBAZI YAPAMBA MOTO HATARI

HATIMAYE BALEKE ABEBESHWA MIZIGO SIMBA…MSIMBAZI YAPAMBA MOTO HATARI

Habari za Simba

Nani mkali wa mabao? Ubishi utamalizika Jumapili hii Uwanja wa Mkapa lakini kwa sasa habari ya mjini ni kuhusu kiwango cha mshambuliaji wa Simba, Jean Baleke.

Amejiunga na Mnyama katika dirisha dogo la usajili na amekuwa moto mkali sio ligi ya ndani pekee hata Ligi ya Mabingwa Afrika huko nako hajapoa.
Tangu Januari 22 alipoichezea Simba mchezo wake wa kwanza dhidi ya Dodoma Jiji pale Uwanja wa Jamhuri ameendelea kucheka na nyavu kama kawaida.

Simba imeshacheza michezo mitano ya Ligi Kuu tangu Januari 22, ikicheza dhidi ya Dodoma Jiji, Singida, Mtibwa Azam FC na Ihefu.

Katika michezo hiyo mitano, Baleke ametupia kambani michezo minne na hakufunga mchezo dhidi ya Azam pekee ambapo zilitoshana nguvu ya bao 1-1 bao la Simba lilitokana na beki wa Azam, Abdalah Kheri kujifunga.

Baleke amefunga mabao saba katika michezo mitano, na mabao matano amefunga kipindi cha kwanza huku mawili akifunga kipindi cha pili kwenye ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Ihefu.

Kwa taarifa yako mabao sita kati ya saba amefunga ugenini huku bao moja pekee ndio amefunga nyumbani katika ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Singida Uwanja wa Makapa.

Bao lake la kwanza alifunga Januari 22 kwenye ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Dodoma ukiwa mchezo wake wa kwanza ndani ya jezi ya Mnyama.

Mabao mengine alifunga Uwanja wa Manungu wakati wakiisambaratisha nyumbani Mtibwa Sugar kwa mabao 3-0 akipiga hat trick na kumfanya mshambuliaji huyo kufikisha mabao saba hadi sasa. Hat trick ya Baleke ndio hat trick pekee iliyofungwa kipindi cha kwanza msimu huu kati ya saba ambazo tayari zimefungwa.

Licha ya kucheza michezo michache ya Ligi Kuu lakini, Baleke anashika nafasi ya tatu katika orodha ya wanaongoza kwa ufungaji kwenye kikosi cha Simba.

Mosses Phiri ndio kinara wa mabao akifunga 10 kama ilivyo kwa Said Ntibazonkiza, John Bocco akifunga mabao tisa akifuata Baleke na Pape Sakho wote wakiwa na mabao saba. Simba hadi sasa ina uwiano wa mabao 46 katika michezo 25 wakati Yanga ikiwa na uwiano wa mabao 39 huku ikiongoza Ligi Kuu kwa alama 68.

SOMA NA HII  MUDATHIR AGEUKA MWIBA HUKO LIGI KUU