Home Habari za Yanga YANGA KUFANYA MATUSI KOMBE LA SHIRIKISHO…LIGI KUU SASA NDIO USISEME

YANGA KUFANYA MATUSI KOMBE LA SHIRIKISHO…LIGI KUU SASA NDIO USISEME

Habari za Yanga SC

BAADA ya ushindi wa bao 1-0 walioupata Yanga, Kocha msaidizi wa timu hiyo Cedrick Kaze amesema wamefanikiwa kuingia hatua ya robo fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika sasa wanawekeza nguvu kutetea mataji yao yote ya Ligi Kuu na Kombe la Shirikisho Afrika (ASFC).

Yanga imeandika rekodi ya kuongoza kundi kwenye mashindano ya Kombe la Shirikisho Afrika kundi D ikifikisha pointi 13 sawa na US Monastir utofauti ukiwa ni mabao ya kufunga na kufungwa.

Akizungumza na SOKA LA BONGO mara baada ya mchezo wao wa mwisho na TP Mazembe uliochezwa jijini Lubumbashi, Kaze alisema umoja uliopo ndani ya timu hadi uongozi ndio siri ya mafanikio waliyoyapata na wanaiona timu yao ikifika hatua kubwa zaidi na kuwashangaza wapenda soka.

“Haikuwa rahisi lakini ni mipango ambayo ilikuwepo kuanzia uongozi, benchi la ufundi na wachezaji ambao wamefanya kile walichoelekezwa na kufanikiwa kufikia lengo ambalo lilikuwa ni moja ya chachu ya kuona tunafika mbali;

“Aina ya timu iliyopo Yanga tunauona mwanga mkubwa kutokana na chachu ya ushindani wa wachezaji kwa wachezaji ambao pia wanatamani kuona wanaandika rekodi kubwa na kuacha historia ndani ya Yanga.”

Kaze alisema wamesahau matokeo yenye rekodi dhidi ya TP Mazembe sasa wanawekeza nguvu mchezo wa ASFC dhidi ya Geita Gold utakaochezwa Aprili 8 ambao amekiri kuwa wapinzani wao ni wazuri lakini wanatakiwa kujipanga kwasababu wao wanahitaji kuweka heshima kwa kutetea mataji yote.

“Geita Gold ni timu nzuri tunatarajia ushindani kutoka kwao kitu pekee naweza kusema ni kwamba tunataka kutetea mataji yetu yote ligi kuu, ASFC tunawaheshimu wapinzani wetu na tunatarajia ushindani.”

Kaze alisema hali ya ushindani wa kikosi na ubora wao inawapa imani ya kuona lolote linaweza kufanyika huku akisisitiza kuwa wao kama benchi la ufundi watafanya kazi yao kwa usahihi na kuwaacha wachezaji wakamilishe kazi yao uwanjani ndani ya dakika 90.

Yanga wakimalizana na Geita Gold ambao wamewafunga nje ndani kwenye ligi kuu watakutana na Kagera Sugar mchezo wa Ligi Kuu Bara utakaopigwa Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, jijini Dar es Salaam.

SOMA NA HII  WAKATI VYUMA VIPYA VIKITAJWA KUTUA ...GAMONDI AWAPIGA MKWARA MASTAA YANGA...