Droo ya hatua ya robo fainali Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho imemalizika nchini Misri kwa timu zinazowakilisha Tanzania Simba na Yanga kujua wapinzani wao.
Yanga ambayo droo yake ilianza mpinzani wake robo fainali ni Rivers United ya Nigeria ambaye alimtoa msimu uliopita katika michuano hiyo.
Mechi hiyo ambayo wachezaji wa Yanga wameiita ni ya kisasi kama itavuka hatua hiyo atakutana na mshindi wa mechi ya Pyramid FC vs Gallant na mechi hiyo itaanzia uwanja wa nyumbani Mkapa.
Mechi ya kwanza kwa Yanga dhidi ya Rivers itapigwa nchini Nigeria kati ya Aprili 21-23 na marudiano uwanja wa Mkapa Aprili 28-30.
Mshambuliaji wa Yanga, Fiston Mayele amesema walitamani kukutana na Rivers United timu ambayo iliwatoa msimu uliopita michuano hiyo na sasa wanakutana tena kwenye robo fainali.
Mayele amesema mechi zilizopita alikosa kucheza dhidi ya timu hiyo na sasa timu hiyo inakwenda kulipa kisasi.
“Mimi binafsi nilikuwa namtaka kwasababu mwaka jana sikupata nafasi ya kucheza naye, tulitolewa mapema watu wakaongea sana kwahiyo tumempata sehemu nzuri,” amesema Mayele