Home Habari za michezo GAMONDI AANZISHA VITA HII YANGA, MASTAA WAHAHA

GAMONDI AANZISHA VITA HII YANGA, MASTAA WAHAHA

KOCHA wa Yanga, Miguel Gamondi ametegeneza vita kubwa kwenye kikosi chake, jambo ambalo litamfanya apasue kichwa kupata kikosi cha kwanza.

Yanga juzi ilicheza mchezo wa kirafiki katika kilele cha Siku ya Mwananchi ilipovaana na Kaizer Chiefs na kufanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 1-0 kweney Uwanja wa Mkapa.

Hata hivyo, pamoja na sehemu nyingine zote kuonyesha kuwa zitakuwa na vita kubwa ya namba, eneo la beki wa kati la timu hiyo linaonekana kuwa na vita kubwa zaidi na kama mabeki wa pembeni hawatakuwa makini watajikuta wakipisha maeneo yao.

Eneo la ulinzi la kati la Yanga lina nahodha Bakari Mwamnyeto, Dickson Job, Ibrahim Bacca na Gift Fred ambaye amesajiliwa kwenye dirisha hili na tayari ameonyesha kiwango cha hali ya juu.

Kuonyesha kuna kazi kubwa kocha huyo katika mchezo huo wa kwanza alianzisha mabeki wawili wa kati , Job na Mwamnyeto ambao ni pacha iliyokuwa inacheza muda mwingi msimu uliopita na kuwatoa wote wakati wa mapumziko.

Baada ya hawa kuondolewa, Gamondi aliwaaingia Bacca ambaye alicheza na Fred na wote wakaonyesha kiwango cha kutisha.

Fred ambaye ni mgeni, alionyesha kuchangamka ambapo kila mpira aliokuwa akiugusa mashabiki wa Yanga walishangilia kuonyesha kuwa wanaikubali kazi yake uwanjani.

Hata hivyo, pacha hizi zitatakiwa kufanya kazi kubwa kwa kuwa wote wana ubora wa hali ya juu na wakiwa wanacheza kwenye timu za taifa lakini wote ni wabishi kwelikweli.

Ubora wao unaweza kuwafanya mabeki wa pembeni kuwa matumbo joto kama ambavyo ilikuwa msimu uliopita wakati ambao kocha Nasreddine Nabi alikuwa anamhamisha Bacca kumpeleka pembeni na wakati mwingine Job kucheza sehemu ya kiungo mkabaji, hivyo lazima wahakikishe wanaonyesha kiwango cha juu zaidi.

Beki wa zamani wa Yanga, Oscar Joshua amesema hili ni eneo ambalo litampasua kichwa kocha huyo, lakini hakuna mazoea kwenye soka kwani yule atakayeelewa haraka mfumo wa kocha ndiye ataanza kikosini.

“Gift ni beki mzuri, lakini kwa ubora wa aliowakuta naona kazi ipo, hapo mwamuzi wa mwisho ni mfumo wa kocha na atakayefanya mazoezi kwa bidii ndiye atakayetoboa nafikiri mwalimu hawezi kuangalia nani alikuwepo awali, ingawa ni sehemu ngumu,” alisema.

Mbali na beki huyo, Williams Mtendawema ambaye naye aliwahi kucheza sehemu ya ulinzi ya Yanga, alisema hapa mwamuzi wa mwisho ni kocha, lakini kuna vita haswa: “Kuhusu eneo la beki wa kati lina wachezaji wazuri, lakini wana kazi ya kumshawishi kocha kwenye mazoezi yao, huku ndiyo sehemu sahihi, hapa kutakuwa na ushindani mkubwa Yanga msimu huu lakini kazi aachiwe mwalimu ingawa hawawezi kucheza wote, mchezaji bora atakaa nje tu.”

SOMA NA HII  NABI AIWAHI YANGA ...AAGANA NA MASHABIKI...ASISITIZA KILA KITU KITAISHA TUNISIA...