Home Habari za michezo YANGA YASHUSHA BEKI HUYU KISIKI KUTOKA SC VILLA

YANGA YASHUSHA BEKI HUYU KISIKI KUTOKA SC VILLA

YANGA YATOA SIRI NZITO USAJILI WA MUSONDA...ULE NI USAJILI WA KIMKAKATI

Klabu ya Yanga imekamilisha usajili wa beki wa kati Gift Fred kutoka katika klabu ya SC Villa kwa mkataba wa miaka mitatu kuitumikia timu hiyo.

Gift ambaye pia ni beki wa timu ya Taifa Uganda anatajwa kumalizana na mabosi wa Yanga kwa ajili ya kuitumikia timu hiyo msimu ujao.

Beki huyu ambaye ni nahodha wa SC Villa amesaini mkataba huo na Yanga akiwa mchezaji huru baada ya mkataba wake kumalizika na Villa mwezi uliopita.

Kabla ya kusaini mkataba huo Gift alikuwa kwenye rada za kuhitajika na timu za Vipers na Kitara FC za Uganda , St George (Ethiopia) na Cape Town (Afrika Kusini).

Mwanaspoti linafahamu Yanga ilikuwa inamfuatilia beki huyo hasa kwenye mchezo wa kufuzu Mataifa ya Afrika (AFCON) kati ya timu ya Taifa Uganda dhidi ya Algeria uliochezwa mwezi uliopita Cameroon.

Habari kutoka Uganda zinaripoti kwamba mchezaji huyo atakuja kujiunga na Yanga muda wowote kutoka sasa na kutangazwa kwa ajili ya kuitumikia timu hiyo msimu ujao.

Gift akitua Yanga atakutana na wachezaji wenzake kutoka Uganda akiwemo Khalid Aucho ambaye alikuwepo huku wengine waliopo kwenye majaribio ni Moses Aliro na Shariph Kimbowa wakitoka katika klabu ya Wakiso Giants na walikuwa kwenye mchezo wa kirafiki dhidi ya Nyasa Big Bullets, Alhamis iliyopita nchini Malawi.

Ujio wa Gift kwenye kikosi cha Yanga ni wazi unaenda kuongeza nguvu katika eneo la ulinzi kwani hapo awali walikuwa wanacheza Ibrahim, Bakari Mwamnyeto, Dickson Job na Yanick Bangala.

Bangala mara nyingine hutumika kama kiungo mkabaji huku upande wa Job yeye akitumika kama beki wa kulia.

Bangala pia inadaiwa anaweza kuondoka kwenye kikosi hicho kwani ameshaonyesha nia ya wazi baada ya kuzungumza kwenye mitandao ya kijamii kwamba ana asilimia 80 za kuondoka na 20 kubaki kikosi cha Yanga.

Upande wa msemaji wa klabu hiyo, Ally Kamwe alikaririwa akisema kila mchezaji ambaye walikuwa wanamuhitaji tayari wameshakamilisha usajili wao.

“Tumeshakamilisha usajili wa wachezaji wetu wote tunaowataka na kilichobaki ni kuwatambulisha tu,”alikaririwa Ally akisema .

Yanga hadi sasa imemtangaza beki wa kushoto ambaye anamudu na kucheza kama winga Nickson Kibabage akiwa ndio ingizo jipya katika timu hiyo.

SOMA NA HII  KUELEKEA AFCON YA TZ, KENYA NA UGANDA....TFF WAITWA MEZANI KUYAJENGA ....