Home Habari za michezo ROBERTINHO AFUNGUKA MBINU ALIZOWAPA WACHEZAJI WA SIMBA

ROBERTINHO AFUNGUKA MBINU ALIZOWAPA WACHEZAJI WA SIMBA

Habari za Simba

KOCHA Mkuu wa Simba, Mbrazili, Roberto Oliveira ‘Robertinho’ amefurahishwa na wachezaji wake wapya waliowasajili kikosini hapo akiwemo Luis Miquissone akibainisha kwamba, wamefiti haraka katika mbinu zake.

Mbali na Luis, Simba imesajili wachezaji wengine kuelekea msimu ujao ambao ni Fabrice Ngoma, Willy Onana, Aubin Kramo, Che Malone Fondoh, Hamis Abdallah, Idd Chilunda, Hussein Kazi na David Kameta ‘Duchu’.

Akizungumza na Spoti Xtra, Robertinho alisema kilichobaki hivi kwake ni kuongezea mbinu chache za kiufundi katika safu ya ushambuliaji pekee zitakazowafanya wachezaji hao wapya wawe bora zaidi.

“Niwaambie mashabiki wa Simba kuwa, kwa sasa tupo tayari kwa mashindano, nawapongeza wasaidizi wangu, tumefanya kazi kubwa kuhakikisha wachezaji wetu wanakuwa timamu kimwili, kiakili na kimbinu jambo ambalo ni muhimu sana kwetu kuelekea msimu ujao.

“Kiukweli haikuwa kazi rahisi, bali utayari wa kila mmoja, hata wale wachezaji wapya walioingia, wamefiti haraka kwenye mifumo na mbinu zetu, ni kitu kizuri kwetu na tunatarajia kuwa na msimu bora zaidi pale mashindano.

“Kilichobaki ni wachezaji wangu kuwaoneshea mashabiki ubora wao uwanjani kwa kuanzia Simba Day ambayo tunakwenda kucheza mchezo wa kirafiki kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar,” alisema Robertinho.

SOMA NA HII  BALEKE AANZA KUANDALIWA MAZINGIRA YA UFUNGAJI BORA, KRAMO ATAJWA