Home Habari za michezo YANGA HII YA GAMONDI SASA HATARI KAMA ULAYA

YANGA HII YA GAMONDI SASA HATARI KAMA ULAYA

Habari za Yanga SC

Klabu ya Yanga haitaki mchezo kwani imeendelea kuwekeza ndani na nje ya uwanja na sasa imegeukia kwenye teknolojia ya kisasa ambayo mastaa wa kikosi hicho wanatumia vifaa ghali mazoezini vinavyotumiwa na wanamichezo mastaa wakubwa duniani wakiwamo mshindi wa tuzo ya Ballon d’Or msimu uliopita, Karim Benzema na mwanariadha Usain Bolt pamoja na mastaa wengine wakubwa duniani.

Kambini Avic Town kumeboreshwa kwa kuweka vifaa vipya vya mazoezi sambamba na kuongeza vingine ambayo awali havikuwapo lakini kubwa zaidi ni kifaa aina ya Electrical Muscles Recovery Stimulation (EMS), ambacho ni kwa mara ya kwanza kwa timu ya Tanzania inatumia kifaa hicho ambacho kinatajwa kuwa ni ghali sana.

Kifaa hicho kilicholetwa kwa msaada wa tajiri wa klabu hiyo kina kazi zaidi ya moja ikiwamo kusaidia kurejesha utimamu wa mwili, kushitua akili na misuli sambamba na kuonyesha sehemu ambazo mchezaji anaweza kuwa ameumia au kupata jeraha bila yeye kujua, na mastaa wamekuwa wakikifurahia kwa kuwa kinautetemesha mwili.

Licha ya kuwapo kimoja lakini kinafanya kazi kubwa ambapo kwa siku kinaweza kutumika kwa wachezaji mmoja hadi watano na kwa kuanzia walianza kutumia Salum Abubakar ‘Sure Boy’, Aboutwalib Mshery na Kibwana Shomary.

Sure Boy akizungumza kuhusu kifaa hicho, alisema ni kizuri kinawafanya wao kama wachezaji kuwa katika hali nzuri baada ya kuvishwa kifaa hicho huku akiweka wazi kuwa kinawatetemesha kwa maumivu lakini mara baada ya kutolewa kinawaacha katika hali nzuri.

“Ubora wa timu unachangia haya yote timu isingekuwa inafanya vizuri sidhani kama haya yote yangefanyika, tunawapongeza viongozi kwa kuendelea kuona umuhimu wa hivi vifaa na tunawaahidi kutowaangusha, tutapambana kuwapa matokeo kiwanjani, ni mara ya kwanza mimi kuona kitu kama hiki,” alisema Sure Boy ambaye alijiunga na Yanga akitokea Azam FC.

“Hiki ni kifaa ghali sana, hata timu za Ulaya siyo zote zinakitumia, ukitafuta kwenye picha za mastaa kama Benzema, Bolt na wengine wengi utaona wamekivaa, kwa hapa nchini hii ndiyo timu ya kwanza inatumia,” kilisema chanzo kutoka mazoezini Yanga.

Ukiachana na hicho pia ‘Wananchi’ wameongeza vifaa vingine ikiwemo kifaa cha kupima uwezo wa mchezaji mazoezini ambacho hupima ufanisi na utendaji kazi wa mchezaji anapokuwa uwanjani.

Chanzo cha kuaminika kutoka ndani ya Yanga kililiambia Mwanaspoti kuwa kwa upande wa vifaa vya kupima uwezo wa mchezaji wamenunua 24 na vimeanza kutoa matokeo kwa wachezaji.

“Kila mchezaji baada ya mazoezi anaonekana ni namna gani amefanya kwa ufanisi unaotakiwa kutokana na kifaa hicho kurekodi matukio na kuonyesha nguvu kazi iliyotumika hivyo inamrahisishia kocha kumpanga mchezaji kutokana na namna anavyo wajibika mazoezini, hiki kilikuwepo mwanzo hata Azam FC, Simba nafikiri wanacho,” kilisema chanzo.

SOMA NA HII  KUMBE PACOME HAMNA KITU