Home Habari za michezo UNAAMBIWA AZIZI KI NDIO KINARA WA MAGOLI YA NAMNA HII

UNAAMBIWA AZIZI KI NDIO KINARA WA MAGOLI YA NAMNA HII

Habari za Yanga SC

Baada ya Stephane Aziz Ki kufunga mabao matatu ‘hat-trick’ katika mechi ya Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Azam FC kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa juzi, akiipa timu yake ya Yanga ushindi wa 3-2, idadi hiyo si tu inamfanya kuwa kinara wa ufungaji kwa sasa, bali ameweka rekodi nyingine mpya.

Katika hat-trick hiyo, bao moja la Aziz Ki, lilitokana na mpira wa kutenga (faulo), hivyo linamfanya kuweka rekodi nyingine ya kuongoza kwa kufunga mabao mengi ya faulo mpaka sasa.

Akizungumza mchezaji huyo raia wa Burkina Faso alisema ‘hattrick’ yake anaitoa zawadi kwa wachezaji wenzake kwa sababu ndiyo waliofanikisha kufanya hivyo, huku akisema siku zote mchezaji mkubwa lazima uonyeshe kitu tofauti katika mechi kubwa kama hizo.

“Nina furaha kufunga ‘hat-trick’ kwenye dabi hii, ukiwa mchezaji mkubwa ni lazima uoneshe kwamba wewe ni mchezaji mkubwa kwenye mechi kama hizo kuanzia kiwango hadi uwajibikaji.

Nayatoa mabao haya matatu kama zawadi kwa wachezaji wenzangu kwa sababu wamenisaidia kunipa nafasi za kufunga,” alisema Aziz Ki.

Mbali na kukaa juu ya kilele cha msimamo wa wafungaji wa Ligi Kuu akiwa na mabao sita na kupiga ‘hat-trick’ yake ya kwanza msimu huu ikiwa ni ya tatu kwenye ligi, zingine zikifungwa na Jean Baleke wa Simba na Feisal Salum ‘Fei Toto’ wa Azam FC, Aziz Ki, pia anaongoza kwa kufunga mabao mengi ya faulo mpaka sasa.

Amefunga mabao mawili kwa njia hiyo kati ya mabao tisa yaliyofungwa kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara mpaka leo hii kwa faulo.

Juzi alifunga bao kwa mkwaju wa adhabu dakika ya 68 na kuipa Yanga bao la pili, kabla ya kufunga lingine la tatu kwa njia ya kawaida. Kabla ya bao la juzi, Agosti 29, alifunga bao la faulo kwenye mechi kati ya Yanga dhidi ya JKT Tanzania likiwa ni la kwanza dakika ya 45 na kuiongoza timu yake kushinda mabao 5-0.

Wachezaji wengine waliofunga mabao ya faulo kila mmoja akifunga moja ni Marouf Tshakei wa Singida Big Stars, Edwin Balua wa Prisons, Tariq Seif wa Geita Gold, Omari Kindamba wa Mashujaa FC, Cheikh Sidibe wa Azam FC, Ibrahim Ajibu wa Coastal Union na Martini Kigi wa JKT Tanzania.

SOMA NA HII  SIMBA WAANZA MAWINDO YA VIFAA VIPYA...MABOSI WA USAJILI WAANZA KAZI KIMYA KIMYA...