Home Azam FC YANGA WAMTISHA DUBE, HUKU NAE AJIBU HILI

YANGA WAMTISHA DUBE, HUKU NAE AJIBU HILI

Mshambuliaji wa Azam FC, Prince Dube amesema mechi ijayo dhidi ya Yanga itakuwa ngumu, lakini Azam haitaingia kinyonge kwa kuwa wanazitaka alama tatu.

Dube ndiye aliyefunga bao pekee lililoipa Azam ushindi wa mwisho mbele ya Yanga katika Ligi Kuu kwenye mechi iliyopigwa Aprili 25, 2021, kabla ya mechi tano zilizofuata baadaye zikiwamo nne za ligi na moja ya Ngao ya Jamii, Yanga kushinda nne na mchezo mmoja kwisha kwa sare.

Akizungumza na Mwanaspoti, Dube alisema anajua matokeo ya mechi zilizopita zitawafanya kuonekana wanyonge mbele ya Yanga, lakini mchezo wa Jumatatu, Azam inataka kumaliza unyonge kwa kupata ushindi. Alisema mchezo huo utakuwa na ushindani mkubwa kwani wamejipanga kuhakikisha wanapata ushindi wa kwanza ndani ya uwanja wa Azam Complex mbele ya wapinzani wao hao.

“Lazima tuendelee kuwa sehemu nzuri katika ligi kwani tuna timu bora yenye wachezaji wazuri. Hatukuanza ligi kwa kasi lakini kwa sasa timu imeendelea kuimarika tunataka kuendeleza kasi.

“Tunajua Yanga ni timu nzuri na hivi karibuni tumekuwa hatupati matokeo mazuri mbele yao, lakini tunahitaji matokeo tofauti kwa timu yetu dhidi yao. Ili uwe bora unahitaji kushinda mechi kubwa kama hizi,” alisema.

Baada ya kupata majeraha kisha kucheza mchezo uliopita Dube sasa amerejea akiwa na afya nzuri.

SOMA NA HII  KISA UMEME KUKATIKA MECHI YA YANGA...MHANDISI MKUU WA UMEME NA WENGINE 7 KWA MKAPA...WAPIGWA CHINI