Home Habari za michezo ‘MAVITUZI’ YA KARABAKA YALIVYOANZA KUJIBU SIMBA KWA HARAKA….’DOGO’ NI BALAAH…

‘MAVITUZI’ YA KARABAKA YALIVYOANZA KUJIBU SIMBA KWA HARAKA….’DOGO’ NI BALAAH…

Habari za Simba leo

KIUNGO mshambuliaji wa Simba, Saleh Karabaka amekuwa na mwanzo mzuri ndani ya kikosi hicho, jambo linalowapa imani wakongwe wa soka kuamini kwamba anaweza kufanya makubwa.

Mchezo wake wa kwanza wa Kombe la Mapinduzi dhidi ya JKU timu yake ya zamani alifunga bao na amefunga tena mechi yake ya kwanza ya Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) dhidi ya Tembo ya Mkoa wa Tabora.

Kiwango alichoonyesha mechi hizo kimemuibua beki wa zamani wa timu hiyo, Frank Kasanga ‘Bwalya’ aliyedai kuwa aina mikimbio, utulivu wa kupiga anapokuwa eneo la kufunga, kasi na umiliki wa mpira ni miongoni mwa ubora alionao.

“Mfano bao alilofunga dhidi ya Tembo ilipigwa pasi na Saido (Ntibanzokiza) lakini mabeki walikuwa mbele yake akatoka nyuma kwa kasi akafunga. Alikuwa na utulivu wa kujua anapiga mpira eneo gani. Kikubwa atulize akili, ajue ukubwa wa Simba na ajifunze kwa wengine hayo yatamfanya afanye vizuri,” alisema.

Mchezaji mwingine wa zamani wa timu hiyo, Mohamed Banka alisema: “Usajili wake haukutikisa. Pamoja na hayo yote naona anajitahidi, asiridhike mapema anapaswa kukaza buti kweli. Kucheza Simba ni nafasi kubwa kwake kukionyesha kipaji chake kwa ukubwa.”

Mkuu wa Idara Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally alisema mbali na Karabaka wachezaji wapya wao wameonyesha wana vitu vya kuisaidia timu.

“Hivyo tunatarajia watafanya makubwa kumalizia msimu huu,” alisema.

SOMA NA HII  MUONEKANO WA UKURASA WA MBELE GAZETI LA CHAMPIONI JUMATANO