Home Habari za michezo HAWA NDIO MAMELOD AISEEE….YANGA WAKICHOMOKA HAPA WAPEWE TU KOMBE LAO…..

HAWA NDIO MAMELOD AISEEE….YANGA WAKICHOMOKA HAPA WAPEWE TU KOMBE LAO…..

Habari za Michezo leo

Yanga imepangwa kukutana na Mamelodi Sundowns katika hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu huu ambapo itacheza mechi ya kwanza kati ya Machi 29 na 30 mwaka huu na mechi za marudiano zitachezwa, Aprili 5 hadi 6 mwaka huu.

Mara ya mwisho kwa timu hizo kukutana ilikuwa ni 2001 ambapo ilikuwa ni katika raundi ya pili ya mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika (wakati huo yakiitwa klabu bingwa Afrika) ambapo Yanga ilitolewa kwa kufungwa mabao 6-5 katika mechi mbili baina yao.

Katika mechi ya kwanza iliyochezwa Afrika Kusini, Mamelodi Sundowns iliibuka na ushindi wa mabao 3-2 na mechi ya marudiano iliyochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, timu hizo zilitoka sare ya mabao 3-3.

Mafanikio ya ndani na nje ya uwanja ya Mamelodi Sundowns hapana shaka ni jambo ambalo limefanya wengi waifuatilie kwa ukaribu na pia kuona kwamba Yanga haina mchezo rahisi dhidi ya timu hiyo ya Afrika Kusini.

Inawezekana baadhi ya mashabiki wa soka nchini hawana wasifu wa kutosha wa Mamelodi Sundowns na kwa kuzingatia hilo, Mwanaspoti inakuletea dondoo kadhaa ambazo zitatoa picha halisi ya mabingwa hao wa Kombe la African Football League (AFL).

Wagumu nyumbani, sio wanyonge ugenini

Mamelodi Sundowns ni miongoni mwa timu ambazo huwa sio rahisi kupoteza mechi kwenye uwanja wao wa nyumbani pindi inaposhiriki Ligi ya Mabingwa Afrika jambo linalochangia kuzipa presha timu nyingi ambazo huenda kukabiliana nayo.

Tangu ilipofungwa mabao 2-1 na CR Belouizdad, Aprili 9, 2021, hadi sasa imecheza mechi 16 mfululizo za Ligi ya Mabingwa kwenye Uwanja wa Loftus Versfeld uliopo Pretoria, Afrika Kusini bila ya kupoteza ikishinda mechi 12 na kutoka sare nne.

Lakini ubabe wa Mamelodi haushii kwa mechi za nyumbani tu bali hata ugenini imekuwa ikifanya vyema na kuthibitisha hilo katika mechi 10 zilizopita za Ligi ya Mabingwa Afrika, imefungwa moja, kutoka sare mbili na kuibuka na ushindi katika michezo saba.

BENCHI LILILOSHIBA

Mamelodi Sundowns ni miongoni mwa timu zenye rasilimali watu za kutosha kwenye mabechi yao ya ufundi ambazo zimekuwa chachu kwao kufanya vizuri katika mashindano mbalimbali inayoshiriki.

Timu hiyo ina jopo la wataalam 24 wanaohusika na idara ya ufundi wakiongozwa na kocha mkuu Rhulani Mokwena huku msaidizi wake akiwa ni Manqoba Mngqithi.

KLABU YA FAMILIA

Familia ya Patrice Motsepe ndio inayoimiliki Mamelodi Sundowns ambapo kwa sasa, mwenye timu, Patrice Motsepe amejiweka kando kuiongoza kutokana na kukabiliwa na majukumu ya Urais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF).

Timu hiyo kwa sasa inaongozwa na mtoto wa Motsepe, Tlhopane Motsepe akisaidiwa na bodi ya wakurugenzi yenye watu sita ambao ni Rejoice Simelane, Freddy Greaver, Andrew Matube, Andre Wilkens, Sandile Langa na Stanley Mabulu.

KIKOSI GHALI

Kwa mujibu wa mtandao wa www.transfermarkt.com, thamani ya kikosi cha Mamelodi Sundowns kinachonolewa na Rhulani Mokwena wa Afrika Kusini ni Euro 33.15 milioni (Sh92.3 bilioni).

Mchezaji ghali zaidi ni Matías Esquivel aliyenunuliwa katika dirisha dogo la usajili, Januari kwa ada ya Euro 2.3 milioni (Sh6.4 bilioni) kutokea Lanus ya Argentina.

Nyota tegemeo wa Mamelodi Sundowns ni makipa Denis Onyango na Ronwen Williams, mabeki ni Rushine De Reuck, Mothobi Mvala, Grant Kekana, Abdelmounaim Boutouil na Khuliso Mudau.

Viungo ni Teboho Mokoena, Thapelo Maseko, Gaston Sirino, Bongani Zungu, Marcelo Allende, Aubrey Modiba, Thembinkos Lorch na Junior Mendieta wakati washambuliaji ni Siyabonga Mabena, Abubeker Nasir na Peter Shalulile.

TIMU YA TAIFA

Timu ya taifa ya Afrika Kusini ‘Bafana Bafana’ ambayo ilifika nusu fainali kwenye fainali za Mataifa ya Afrika (Afcon) 2023 iliyofanyika Januari mwaka huu huo Ivory Coast, iliundwa na wachezaji 10 kutoka Mamelodi. Kati yao, wachezaji sita walikuwa ni wa kikosi cha kwanza kilichomaliza katika nafasi ya tatu ya michuano hiyo mikubwa zaidi kimataifa kwa Afrika.

SOMA NA HII  AFCON 2023....TANZANIA KUFUNGUA DIMBA NA MOROCCO...KUMALIZA KAZI NA KINA MAYELE...