SINGIDA BLACK STARS YAMFUNGIA KAZI MSAUZI
Singida Black Stars imeanza mipango ya kuimarisha kikosi chake kwa ajili ya msimu ujao kwa kuweka macho kwa kiungo mshambuliaji wa Golden Arrows ya Afrika Kusini, Siyanda ‘Skhwishi’ Ndlovu.
Taarifa zinaeleza viongozi wa Singida Black Stars wanatafakari kufungua mazungumzo rasmi na mchezaji huyo pamoja na klabu yake ili kuona uwezekano wa kumleta Tanzania dirisha lijalo la usajili.
Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa timu hiyo kuongeza ubora wa kikosi chake hasa katika maeneo ya pembeni ambako wamekuwa wakicheza, Lamine Jarjou na Mossi Nduwumwe.
Ndlovu ambaye amefunga mabao manne na kutoa asisti sita katika ligi ya Afrika Kusini msimu huu, amekuwa akitajwa kuwa miongoni mwa viungo washambuliaji wenye uwezo mkubwa wa kucheza nafasi mbalimbali za ushambuliaji ikiwemo winga ya kushoto na kulia.
Hata hivyo, Singida BS inaweza kukutana na ushindani mkali katika mbio za kuwania saini ya Ndlovu kutokana na taarifa kuwa klabu mbili kutoka Morocco tayari zimeonesha nia ya kutaka huduma ya kiungo huyo.
Mbali na klabu hizo za Morocco, pia kuna timu kadhaa za Afrika Kusini zinazotajwa kuwa nyuma ya dili hilo.
Iwapo Singida BS itafanikiwa kukamilisha usajili huo, itakuwa imeongeza kiungo mshambuliaji mwenye uzoefu wa kucheza katika mazingira ya ushindani wa juu. Hilo linaweza kuipa timu nguvu zaidi katika harakati za kupambana kwenye mashindano mbalimbali msimu ujao.