Home Uncategorized UD SONGO WALIISHINDA SIMBA KWA KUTUMIA SILAHA ZA SIMBA, WAKATI WA KUNYANYUKA...

UD SONGO WALIISHINDA SIMBA KWA KUTUMIA SILAHA ZA SIMBA, WAKATI WA KUNYANYUKA NA KUSONGA MBELE NI SASA


SIMBA Jana imetolewa rasmi kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwenye uwanja wao wa nyumbani ambao msimu uliopita walifanya maajabu makubwa yaliyoushangaza ulimwengu.

UD do Songo wamewafundisha Simba kwamba hata wao walikuwa wana nafasi ya kupata ushindi kwenye mchezo wa kwanza nchini Msumbiji.

Wengi hawakuamini kwamba inawezekana kwa Simba kutolewa hasa ikiwa nyumbani tena uwanja wa Taifa ila mwisho wa siku matokeo yameamua na kila mmoja kavuna kile alichokipanda.

Kuna vingi vya kujifunza kwa sasa wakati huu kwa Simba wenyewe, mashabiki na wachezaji namna ya kuamini kwamba mpira ni sayansi na sio maneno.

Hakuna ambaye haamini kwamba Simba ilicheza mpira mzuri mwisho wa siku ikaambulia sare ambayo haina manufaa kwao kutokana na wageni kupata bao la mapema lililodumu mpaka dakiza ya 87.

Hapo tunaona kwamba kikubwa ambacho kinaugawa mchezo wa mpira ni ushindi na muda wa kuupata ushindi na ndio maana kuna wakati nilipokuwa nikizungumza na Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Assems aliniambia kwamba kupata ushindi wa mapema ni silaha kwa timu.

“Kama timu itaanza kwa kushambulia na kuleta presha kubwa kwa wapinzani ni rahisi kwetu kupata ushindi mapema na kuleta presha kwa wapinzani wetu.

“Michezo mingi ya msimu uliopita nikiwa nyumbani nilikuwa nawaambia wachezaji wangu wanapaswa wapambane wafunge mapema na nilikuwa ninagawa mchezo kwa dakika kuanzia ile ya kwanza mpaka ya 45,” alisema.

Hii ndio silaha kubwa ya Smba ambayo ilivuja upande wa pili kwa wapinzani wao na wakaitumia kutafuta matokeo mapema uwanja wa Taifa.

Bao ambalo walilipata dakika ya 14 kupitia kwa nahodha wao Luis ilikuwa ni moja ya ngao ambayo Simba wamekuwa wakiitumia wakiwa uwanja wa nyumbani na ndio maana ilikuwa ngumu kupata dawa mapema kwa kuwa walijiamini wakasahau kwamba wana kazi ngumu ya kutafuta bao la kusawazisha mapema.

Licha ya Simba kuugawa mchezo kwa wakati mzuri ilishindwa kumaliza nafasi ambazo imetengeneza na kuruhusu kufungwa bao la mapema jambo ambalo ni mbinu kubwa ya Aussems, Kocha wa Simba hapo ndipo ugumu ulipoanzia.

Mchezo ulikuwa ni wa wazi kwa timu zote na rekodi zinaonyesha kwamba Simba ilimiliki mpira kwa asilimia 65 huku wapinzani wakimiliki asilimia 35 jambo jema kwa Simba lakini lina maumivu kwa kuwa umiliki wa mpira haujawasaidia.

Mbali na hilo pia hata idadi ya mashuti yaliyolenga langoni Simba ilipiga jumla ya mashuti matano huku wapinzani wao wakipiga mashuti matatu, katika hayo kwa Simba moja ndio lilizama langoni na manne hayakuzaa matunda bado kuna kitu cha kujifunza.

Kwa sasa mashabiki wa Simba, viongozi pamoja na wadau ni muda wa kutafakari pale mlipokosea na kujipanga kwa ajili ya msimu ujao maisha lazima yaendelee.

Kama ni kupoteza kwa sasa mmepoteza na dira kwa kiasi fulani itakuwa imezima kwani malengo ya kufika hatua ya robo fainali yameishia hapa, hampaswi kupoteza matumaini.

SOMA NA HII  HIZI HAPA DAKIKA 450 ZA MOTO KWA MBELGIJI WA YANGA, RATIBA YAKE BALAA, BANDIKA BANDUA