Home Uncategorized YANGA CHINI YA LUC YAWEKA REKODI YA AJABU

YANGA CHINI YA LUC YAWEKA REKODI YA AJABU


YANGA imekubali kipigo cha pili mfufulizo baada ya kufungwa na Azam FC katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam juzi.

Bao pekee katika mchezo huo lilifungwa dakika ya 26 baada ya kipa wa Yanga, Farouk Shikhalo kupangua kona iliyopigwa na Bruce Kangwa na mpira kuanguka miguuni mwa Ally Mtoni ‘Sonso’ na kujifunga.

Mchezo huo ambao ulikuwa ulichezwa mvua ikinyesha ulishuhudia dakika ya 76 Yanga wakipata pengo baada ya beki wao Ally Mtoni kuonyeshwa kadi nyekundu baada ya kumchezea rafu ya makusudi beki wa Azam FC, Nickolas Wadada.

Azam FC ni kama wamelipa kisasi kwani msimu uliopita walikubali kichapo cha mabao 2-1, mchezo uliochezwa Uwanja wa Azam Complex na kufungwa tena 1-0 katika mchezo wa marudiano kwenye Uwanja wa Uhuru.

Huu ni mchezo wa pili mfululizo Yanga kufungwa baada ya kufungwa na Kagera Sugar kwa mabao 3-0 nyumbani Uwanja wa Uhuru, wakati Azam FC waliifunga Lipuli kwa mabao 2-0 mchezo uliochezwa katika Uwanja wa Taifa.

Kipigo hicho kinaifanya Yanga kuzidi kuwa mbali na Simba, ambayo mchezo uliopita ilishinda kwa mabao 2-1 dhidi ya Mbao FC kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza ambapo pia jana iliitwanga Alliance mabao 4-1.

Kwa matokeo hayo sasa Yanga imebaki katika nafasi ya nane ikiwa na pointi 25 baada ya kucheza michezo 14 wakati Azam imepanda nafasi ya pili kwa pointi 32 baada ya kucheza michezo 15.

Kikosi cha Azam FC kilikuwa ni Razak Abalora,Nickolas Wadada, Bruce Kangwa, Daniel Amoah, Oscar Masai, Bryson Raphael, Joseph Mahundi, Salum Abubakar, Shabaan Chilunda, Obrey Chirwa na Idd Seleman.

Yanga ni Farouk Shikhalo, Juma Abdul, Jafary Mohamed, Lamine Moro, Ally Mtoni, Pappy Tshishimbi, Deus Kaseke, Haruna Niyonzima, Mapinduzi Balama, David Molinga na Patrick Sibomana.

Imeandaliwa na Rahel Pallangyo
SOMA NA HII  KOCHA MPYA YANGA AMEANZA KAZI