Home Uncategorized FRAGA AWEKA AHADI NYINGINE SIMBA

FRAGA AWEKA AHADI NYINGINE SIMBA


KIUNGO mkabaji wa Simba, Mbrazili Gerson Fraga, ametamba kwamba ataendelea kufunga mabao kwenye ligi kila mara atakapokuwa akipata nafasi ya kuanza ndani ya kikosi hicho.

Mbrazili huyo amejinasibu hivyo baada ya kufunga mabao mawili wakati Simba wakishinda 2-0 kwenye mechi ya Ligi Kuu Bara iliyopigwa katika Uwanja wa Taifa, Dar.

Mabao ya Mbrazili huyo yameifanya Simba kuendelea kukaa kileleni mwa msimamo wa ligi, wakifikisha pointi 44.

Fraga mwenye mabao matatu kwenye ligi, amesema kwamba anajisikia furaha kuona amefunga mabao hayo lakini ataendelea na suala hilo endapo atapata nafasi ya kucheza.

“Ni kitu kizuri kuona nimefunga na nimeisaidia timu yangu kushinda mechi ile. Nimefunga haya mabao kwa ajili ya timu na nimefanya kwa ubora wangu baada ya kupata nafasi ya kucheza.

“Unajua pale unapocheza unatakiwa kutimiza majukumu yako kwa kiwango cha juu kama nilivyofanya licha ya kwamba mimi ni mkabaji lakini nimepata nafasi nikafunga na nitafanya hivyo kwenye mechi zijazo,” alisema Fraga ambaye pia alifunga kwenye mechi ya Kombe la Shirikisho (FA) dhidi ya Arusha FC (AFC).
SOMA NA HII  SPURS YACHAPWA NJE NDANI NA CHELSEA