Home Uncategorized MBELGIJI SIMBA ATOA SABABU ZA TIMU YAKE KUBORONGA KIWANGO

MBELGIJI SIMBA ATOA SABABU ZA TIMU YAKE KUBORONGA KIWANGO


MASHABIKI wa Simba wameonyesha hasira huku wakidai hawaelewi kinachoendelea kwenye timu yao haswa kwenye kiwango na aina ya matokeo.

Lakini kocha mkuu wa timu hiyo, Mbelgiji, Sven Vanderboeck amesema hata kubana kwa ratiba kunachangia.

Kocha huyo amesema hayo kutokana na ushindi wa mabao ya dakika za mwisho ambayo walioupata kwenye mechi dhidi ya Mwadui, Namungo na juzi Jumanne dhidi ya Polisi Tanzania.

“Unapocheza kila baada ya siku mbili kama ambavyo ilivyo kwetu, inapofika kipindi cha pili pale ndiyo mnakuwa na nguvu kubwa sana ya kupata ushindi ndiyo maana unaona inakuwa hivyo kwetu.

“Tuna ratiba ambayo haitupi muda wa kutosha kupumzika kwa hiyo ni lazima tuwe tunapambana kupata ushindi dakika za mwisho, lakini kitu kingine kinachochangia kushinda dakika za mwisho ni kwa sababu ya kufungwa mapema.

“Tunapofungwa mapema tunazidisha juhudi ya kufunga na nina safu nzuri ya washambuliaji ambao wanafanya kile ninachokitaka. Japo hali hii siifurahii sana kwa sababu ninataka tumalize mechi kabla ya kufika muda huo,” alisema.

Katika hatua nyingine, habari za ndani kutoka Simba zinasema kuwa, kocha huyo amewapiga pini wasaidizi wake wote akiwemo kocha mzalendo, Seleman Matola, kuzungumza jambo lolote bila ya ruhusa maalum tofauti na ilivyokuwa awali.

AJIBU ATAJWA

Sven ametamka kuwa sasa ameanza kumuelewa kiungo wake mshambuliaji Ibrahim Ajibu ambaye juzi alitokea benchi na kuisaidia timu yake kupata ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Polisi Tanzania.

“Alipoingia Ajibu timu ilionekana kubadilika kwa timu kushambulia goli la wapinzani baada ya kufanyia maelekezo yangu vizuri na yeye nilimtaka kuwalazimisha mabeki kuingia ndani ya 18 ndiyo kitu ambacho alichokifanya kabla ya kufunga bao.

“Ninataka wachezaji wa aina hii ya Ajibu anayecheza kwa kufuata maelekezo yangu kama ilivyokuwa yeye, kuingia kwake kulibadilisha timu nzima kutokana na uwezo wake wa kumiliki mpira huku akilazimisha mashambulizi.

“Nilimuingiza Ajibu baada ya kumuona (Francis) Kahata, (Clatous) Chama wote wamechoka ambao nilikuwa nawategemea katika mchezo huu, hivyo nimpongeze kwa kuiwezesha timu kupata matokeo mazuri.”
SOMA NA HII  SIMBA YAPANIA KUIBUKA NA USHINDI MBELE YA MWADUI FC