Home Uncategorized WACHEZAJI MSIJISAHAU KUSIMAMA KWA LIGI LAZIMA MLINDE VIPAJI VYENU, TAHADHARI YA CORONA...

WACHEZAJI MSIJISAHAU KUSIMAMA KWA LIGI LAZIMA MLINDE VIPAJI VYENU, TAHADHARI YA CORONA MUHIMU


HOFU kubwa kwa sasa imetawala kila kona ya dunia kutokana na kusambaa kwa Virusi vya Corona ambavyo vilianza kusambaa mwezi Desemba mwaka jana nchini China.
Tunaona kwamba Ligi Kuu Bara imesimamishwa kwa muda wa mwezi mmoja ili kupisha kusambaa kwa virusi vya Corona.
Jambo kubwa linalotakiwa kwa sasa ni kuona kwamba tahadhari inachukuliwa na kila mmoja bila kujali nani anauwezo mkubwa ama hana uwezo kwani afya ni jambo la msingi kuliko kitu chochote.
Tayari Tanzania pia imeripotiwa waathirika kadhaa wamapatikana hii pia imeongeza hofu kubwa kwa watanzania kitu ambacho ni hatari kuliko tunavyofikiria.
Cha msingi ni kuona kwamba kila mmoja anatimiza majukumu yake kwa kufuata kanuni za afya zinazotolewa na Serikali pamoja na vituo vya afya.
Haya yote ambayo tunaambiwa tuyafanye kwa sasa ni mambo ambayo tumekuwa tukiyafanya siku zote lakini ilikuwa sio kwa kumaanisha sana bali kwa mazoea.
Kwa imani zetu tusisahau kumwomba Mungu atuepushe na janga hili ambalo linapita kwa kuwa kila kitu yeye anajua namna ya kutulinda watu wake na kutufanya tuwe salama.
Familia ya michezo duniani kote imepigwa ganzi kutokana na kushindwa kuendelea na shughuli zote zinazohusu michezo kwani mikusanyiko yote imezuiwa na hakuna namna nyingine kwa sasa ya kufanya.
Ligi Kuu Bara, Ligi Daraja la Kwanza , Ligi Daraja la Pili, Ligi ya Wanawake, Ligi ya Mabingwa wa Mkoa nayo pia imesitishwa kwa muda.
Wakati huu maisha inabidi yaendelee huku tahadhari zikichukuliwa kwa wachezaji na watu wa soka kwani kusimamishwa kwa ligi haina maana kwamba itasimama milele.
Kuna ulazima kwa wachezaji kuendeleza utamaduni wa kulinda vipaji vyao wakiwa nyumbani bila kusahau kwamba wanapaswa kulinda familia zao kwa ajili ya kuwalinda na Virusi vya Corona.
Endapo wachezaji watajisahau na kuendelea kuishi bila kufikiria kulinda vipaji vyao itawapa wakati mgumu wa kurejea kwenye ubora wao ambao walikuwa wameanza kuonyesha.
Ndanda FC ya Mtwara walianza kuonyesha ubora wao kwa kuanza kujinasua taratibu kutoka kwenye mstari wa timu tano za chini huku KMC nao wakishinda mechi zao nne mfululizo kwa mwezi Machi.
Kusimama kwa ligi kutawapa manufaa wachache huku wengine wakiishia kwenye maumivu iwapo watashindwa kurudi kwenye gia ambayo walikuwa wameianza.
Ushindani ni mkubwa pande zote ikiwa ni pamoja na kwa timu ambazo zinataka kupanda daraja kutoka Ligi Daraja la Kwanza mpaka zile ambazo zinataka kushuka daraja kutoka Ligi Kuu Bara.
Nina amini muda wa mwezi mmoja kwa wachezaji na viongozi ni mkubwa iwapo watakuwa makini katika kulinda vipaji vyao na kuendelea kufanya mazoezi kwa wakati ili watakaporejea waendelee pale walipoishia.
SOMA NA HII  KUELEKEA MECHI NA SIMBA..MO BANKA AIPA NGUVU YANGA