Home Uncategorized YANGA YA GSM WAIFUATA SAINI YA ‘KIBERENGE’ CHA AS VITA YA CONGO

YANGA YA GSM WAIFUATA SAINI YA ‘KIBERENGE’ CHA AS VITA YA CONGO

KATIKA kuhakikisha wanafanikiwa kunasa saini ya winga wa As Vita, Tuisila Kisinda, uongozi wa Yanga unatarajia kutuma mwakilishi kwenda Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), ili kukamilisha mchakato wa usajili.

Taarifa za uhakika kutoka ndani ya Yanga zinasema tayari wameshajiandaa kumtuma kiongozi mmoja kwenda DRC kumsajili Kisinda kama ilivyopendekezwa na Kocha Mkuu, Luc Eymael.

“Kiongozi mmoja wa GSM anatarajia kusafiri kuelekea Congo, tunasubiri hii corona iishe, kwani tunahitaji kwenda kumalizana na Kisinda, nyota huyo ni mapendekezo ya kocha mwenyewe na pia tutasajili wachezaji wengine wanne wa kimataifa,” kilisema chanzo chetu.

Kiliongeza nafasi alizopendekeza kocha huyo ya mshambuliaji, winga, kiungo na beki na tayari mdhamini wao anasimamia masuala ya usajili na kuendelea vizuri na mazungumzo na baadhi ya wachezaji wa ndani.

“Wachezaji hao wengine, tutawataja muda ukifika, kwa sababu sasa sio busara kutaja majina yao kutokana na mambo bado yako mwanzoni, ” aliongeza kiongozi huyo.

Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Frederick Mwakalebela aliliambia gazeti hili mchakato wa usajili unaendelea ‘kimya kimya’ na watahakikisha wanawanasa wachezaji waliopendekezwa na benchi la ufundi.

Bado Yanga haijakata tamaa ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Bara kwa sababu inaamini kwenye soka lolote linaweza kutokea katika mechi 10 zilizosalia za watani zao, Simba.

SOMA NA HII  YANGA KUISHUSHA SIMBA KILELENI