Home Uncategorized LALA SALAMA INAHITAJI MAAMUZI MAKINI KWA SASA, MAMBO BADO HAYAJAWA SHWARI

LALA SALAMA INAHITAJI MAAMUZI MAKINI KWA SASA, MAMBO BADO HAYAJAWA SHWARI


MAAMUZI makini ndani ya uwanja kwa waamuzi wetu wa Ligi Kuu Tanzania Bara pamoja na Ligi Daraja la Kwanza kwa wakati huu yanatakiwa ili kuongeza hamasa ya mashabiki kuzidi kujitokeza ndani ya uwanja.
Mbali na mashabiki pia hata wachezaji wakati mwingine wanapoteza ile nguvu ya asili ya kupambana uwanjani licha ya kwamba wanashauriwa wao wasicheze na refa bali wacheze mpira.
Kumekuwa na kasumba ya waamuzi kufanya mambo ambayo kwa macho yanaleta mkanganyiko kwa wachezaji pamoja na mashabiki wanaofuatilia masuala ya michezo.
Hali hii haipo kwenye Ligi Kuu Bara pekee mpaka Ligi Daraja la Kwanza kumekuwa na matokeo ambayo hayaridhishi hasa kwa waamuzi kushushiwa lawama kwamba wanashindwa kufuata sheria 17.
Wakati masuala ya michezo yalipokuwa kwenye harakati za kurejea Shirikisho la Soka Tanzania,(TFF) lilitoa taarifa kwamba waamuzi wote wamelipwa stahiki zao ambazo walikuwa wanadai awali.
Jambo hili lilitoa picha kwamba kutakuwa na haki na waamuzi hawatakuwa na mawazo mengine wakati wa kuchezesha mechi zao ila mambo yamekuwa tofauti na vile ambavyo watu walifikiria.
Tayari mechi zaidi ya mbili zimekuwa na malalamiko kwamba waamuzi wanashindwa kwenda na kasi ya mpira. Kukosea sio kosa ila pale ambapo makosa yanajirudia ina maana hakuna kinachofanyiwa kazi hivyo ni muhimu kwa waamuzi kutazama upya namna bora itakayowarejesha kwenye umakini.
Mechi ya Yanga dhidi ya Mwadui iliyochezwa Uwanja wa Kambarage kulikuwa na goli lilofungwa na Yanga likakataliwa ikaelezwa kuwa ni la kuotea maisha yakaendelea Yanga ilishinda bao 1-0.Mchezo mwingine ambao umekuwa ukizungumzwa sana ni ule wa Yanga na Azam FC.
Hapa kinachosababisha mechi hii kuzungumzwa sana ni ukubwa wa timu zote mbili hivyo ina maana kwamba dunia inafuatilia na kila mmoja anahitaji kujua kwamba ni namna gani maisha yanaendelea kwenye ulimwengu wa soka.
Inaumiza kwa mashabiki na wachezaji pale wanaposhindwa kupata kile ambacho wanafikiria hii ni ngumu kueleweka kirahisi hasa matukio yanapotokea kwa kufuatana.
Kwenye mchezo wa Yanga  na Azam uliochezwa Uwanja wa Taifa, Juni 21 penalti mbili moja kwa Yanga na moja kwa Azam zilipita kama upepo huku mabao mawili yaliyofungwa na Azam FC yote ikilelezwa kuwa ni ya kuotea.
Katika hili ni wazi kwamba sheria 17 lazima zifuatwe na ikiwa zitapindishwa kuna maumivu ambayo timu zinapata kwa namna moja ama nyingine.
TFF katika hili kuna umuhimu wa kuwekeza mara dufu kwenye sekta ya waamuzi ili kupata matokeo mazuri hapo baadaye kwenye nyanja za michezo kwa Bongo.
Ikumbukwe kuwa timu zote ambazo zinangia ndani ya uwanja zinawekeza fedha nyingi kabla ya kuingia uwanjani na furaha ya malipo yao ni ushindi ama mchezo wa haki bila lawama.
Hivyo ili kumaliza haya kuna ulazima wa umakini kuongezeka na kutazama namna gani kila timu inapata ushindi halali huku sheria 17 zikipewa kipaumbele katika maamuzi ya waamuzi.  
SOMA NA HII  Alichokisema Amunike leo.