Home Uncategorized MTIBWA SUGAR YAZITAKA POINTI TATU ZA AZAM FC

MTIBWA SUGAR YAZITAKA POINTI TATU ZA AZAM FC


ZUBER Katwila, Kocha Mkuu wa Mtibwa Sugar amesema kuwa wachezaji wake wapo tayari kwa ajili ya mchezo wao unaofuata wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Azam FC unaotarajiwa kuchezwa Julai 15 Uwanja wa Gairo, Morogoro.


Mtibwa Sugar itawakaribisha Azam FC wanaonolewa na Arstica Cioaba wenye kasi ya kusaka ushindi ili kubaki nafasi ya pili huku Mtibwa Sugar ikiwa na uhitaji wa pointi tatu kujinusuru kushuka daraja.

Mchezo wao wa ligi uliopita Mtibwa Sugar ilipoteza kwa kufungwa bao 1-0 mbele ya Mbao FC Uwanja wa Kirumba huku Azam FC ikitoka kushinda mbele ya Mwadui FC bao 1-0.

Katwila amesema kuwa kupoteza pointi tatu haina maana kwamba timu haina uwezo bali ni makosa ambayo wanayafanya hivyo watayafanyia kazi.

“Tumefungwa hilo lipo wazi ila haina maana kwamba hatuna uwezo nguvu tunazo na tunaweza kuleta ushindani kikubwa ni kwamba makosa tuliyofanya yametugarimu kwa sasa tunayafanyia kazi.

“Kwa sasa tunajiandaa na mchezo wetu dhidi ya Azam FC ambapo tutakuwa nyumbani, tutakachokifanya ni kuweza kupambana kupata pointi tatu muhimu ambazo zitatupa nafasi ya kujinasua pale tulipo kwani tupo kwenye nafasi mbaya,” amesema.

Mtibwa Sugar ipo nafasi ya 16 ikiwa na pointi 38 baada ya kucheza mechi 34 huku Azam FC ikiwa nafasi ya pili na pointi 65 baada ya kucheza mechi 34.
SOMA NA HII  YANGA HAWAPOI WAJIBU DONGO LA SIMBA KWA VITENDO, CHEKI JIBU LAO LAZIMA UKAE