Home Uncategorized ONYANGO: KAHATA KANILETA SIMBA SC

ONYANGO: KAHATA KANILETA SIMBA SC

 


KITASA kipya cha Simba, Joash Onyango raia wa Kenya, amefunguka kuwa kiungo mshambuliaji wa timu hiyo, Francis Kahata ndiye aliyemleta klabuni hapo kutokana na kuwasiliana naye kabla ya kumwaga wino wa kuitumikia timu hiyo.

 

Onyango ameongeza kwamba licha ya kuwasiliana na Kahata, pia mwenyewe alikuwa anataka kubadilisha upepo ndiyo sababu akakubali kutua Simba kwa ajili ya msimu ujao wa 2020/21.


Mkenya huyo juzi Ijumaa alisaini mkataba wa miaka miwili wa kuitumikia Simba akitokea Gor Mahia ya Kenya.

 

Onyango amesema kwamba alikuwa anafanya mawasiliano muda mrefu na Kahata anayecheza naye timu ya taifa ya Kenya, Harambee Stars na ndiye ambaye amemvuta kuja Tanzania na kutua Simba.

 

“Kwanza mimi kuja Tanzania nilikuwa nataka kupata changamoto mpya baada ya kucheza Gor Mahia kwa miaka minne ndiyo maana nikaondoka na kuja kusaka changamoto mpya. “Nilikuwa nawasiliana na Kahata kabla ya kuja hapa na alikuwa ananiambia nikija mambo yatakuwa mazuri.

 

“Kabla ya kusaini hapa Simba, Yanga walinifuata na kufanya mazungumzo nao lakini hatukufika mbali kwa sababu mtu ambaye nilikuwa naye wa Simba alinifanya nisaini kwao na kuachana na wengine,” alimaliza Mkenya huyo.

Stori: SAID ALLY,Dar es salaam

SOMA NA HII  POGBA AKUTWA NA VIRUSI VYA CORONA