Home Uncategorized KAULI YA MZAHA YA MANARA INAYOFANANA NA ILE YA KIUFUNDI YA KOCHA...

KAULI YA MZAHA YA MANARA INAYOFANANA NA ILE YA KIUFUNDI YA KOCHA YANGA

 


NA SALEH ALLY

HAJI Manara huonekana ni mtu mwenye utani wakati wote, hii inatokana na yale maneno yake ya shombo katika mitandao ya kijamii au pale anapokuwa anazungumza na waandishi wa habari.


Manara amekuwa akiwacharua sana mashabiki wa Yanga na huenda ndiye mtu anayeonekana kuwa kero kubwa kwa mashabiki wa Jangwani.


Kiasili yeye baba yake ni mchezaji mkubwa wa zamani wa Yanga, hapa ninamtaja Sunday Manara lakini mwanaye amegeuka kuwa kero kubwa kwa mashabiki wa klabu hiyo. Na hii ndio raha ya Yanga na Simba.


Kutokana na mambo yake ya utani, Manara amekuwa akionekana karibu kila anachozungumza ni kitu kilichojaa masihara tu licha ya kwamba amekuwa anazungumza mambo mengi kwa wasikilizaji walipaswa kuyaweka katika nidhamu.


Nasema yawekwe katika nidhamu kwa maana ya kutafuta kipimo. Pamoja kwamba Manara huzungumza kwa masihara sana lakini amekuwa na mengi yanayoweza kutumika kutafakari na kuusaidia mpira wetu.


Manara ni mtu anayeujua mpira hasa wa Tanzania, anajua vitu vingi na bahati nzuri amejaaliwa katika kuhifadhi kumbukumbu na kwa kumbukumbu zangu, Manara ni kati ya wachambuzi wa mwanzoni kabisa wa mpira hapa nyumbani.


Hivi karibuni, alitoa kauli akiwaonekana kama anawatania Yanga kwamba wawe makini sana kwa kuwa wakati Simba wakiwa wanajiandaa kama zilivyo timu nyingine, wao walikuwa “wanazurura”.


Inawezekana kabisa neno kuzurura linaweza likawa lilitengeneza mzaha lakini alichokuwa akimaanisha Manara ni kwamba Yanga hawakuwa wameanza mazoezi katika ile hali iliyoonyesha umakini kwa maana ya mazoezi ya mwanzoni mwa msimu.


Pre season ndio kipindi cha kujaza tank. Ujazaji wake unakuwa hivi, kujiandaa na kuifanya timu kuwa imara mapema. Hivyo kama utaanza maandalizi mwanzoni bila kufuata misingi ya uhakika, basi ujue mambo hayatakaa sawa hata baadaye.


Hapa Manara akaingiza mzaha mwingine, kwamba andaeni malalamiko yenu mapema msije mkaanza kusema Simba inapendelewa.



Hapa unaona kuna kitu kingine cha kutulia na kutafakari, maana unaweza kuwaza kuwa unaonewa maana una kikosi vizuri kwa maana ya mchezaji mmojammoja. Lakini unaona mambo si mazuri.

SOMA NA HII  LIVE: YANGA 1-0 RUVU SHOOTING


Baada ya mechi dhidi ya Prisons ya Mbeya ambayo iliisha kwa sare ya bao 1-1, Kocha Mkuu mpya wa Yanga, Zltatko Krmpotic amesema kuwa anaona wachezaji wake walikuwa hawana uwezo wa kumaliza dakika 90. Hii maana yake, matanki yao hayakuwa yamejaa vizuri na hiki ndicho alichokisema Manara kwa njia ya mzaha.


Maana yake nini, maandalizi ya mwanzo wa msimu kwa kauli ya Manara na Krmpotic hayakuwa sahihi, yalikuwa na walakini na lazima yarekebishwe.


Kocha huyo raia wa Serbia ameomba apewe mechi tatu kuweza kurekebisha mambo na kukiweka kikosi chake katika mwendo ulio sahihi.


Ndio maana nikaona niwakumbushe kwamba si kila la Manara ni mzaha kwa kuwa alichokisema siku chache kimejidhiirisha lakini kocha wa Yanga amelizungumza kiufundi na lazima mashabiki wampe nafasi kocha huyo akianza kazi ili kuhakikisha kikosi chao kinakaa sawa kwa kuwa kina wachezaji wazuri kutokana na usajili mpya lakini muunganiko, haujakaa sawa.


Anayepaswa kufanya kazi hii ya muunganiko ni Krmpotic na kama ilivyo kawaida, mabadiliko katika mpira hayawezi kuwa kama kupanda baiskeli tu na kuanza kuendesha. Wakati mwingine vitu vinahitaji subira kwa maana ya muda ili kubadilishwa sahihi.


Tayari Krmpotic kaliona tatizo, hili ni jambo sahihi kabisa. Tayari ameanza kulitibu tatizo, hili ndilo la uhakika zaidi. Hivyo aaminiwe ili aweze kufanya anachoona ni sahihi kutibu hilo lililosemwa na Manara na baadaye yeye baada ya kukiona kikosi kikicheza mechi ya kwanza ya ligi.