Home Uncategorized MBEYA CITY BADO HAIJAPOTEZA MATUMAINI VPL

MBEYA CITY BADO HAIJAPOTEZA MATUMAINI VPL


 AMRI Said, Kocha Mkuu wa Mbeya City amesema kuwa wachezaji wake hawajapoteza matumaini ya kupata ushindi kwenye mechi zake zinazofuata licha ya kupoteza mechi zote mbili mfululizo.

Mbeya City imeanza Ligi Kuu Bara kwa kuchechemea baada ya kufungwa mfululizo mechi zake zote mbili ambazo ni dakika 180 ikiwa ugenini.

Ilianza kupokea kichapo cha mabao 4-0 mbele ya KMC Uwanja wa Uhuru ilikuwa Septemba 7 kisha ikapoteza mbele ya Yanga, Uwanja wa Mkapa, Septemba 13 kwa kufungwa bao 1-0.

Akizungumza na Saleh Jembe, Said amesema kuwa ushindani ndani ya ligi ni mkubwa ana imani ya kufanya vizuri kutokana na aina ya wachezaji alionao kwenye mechi zake zijazo.


“Tulianza kwa kupoteza mchezo wetu wa kwanza, makosa ambayo tuliyafanya niliyaona na nikayafanyia kazi. Kitu kizuri ni kwamba wachezaji walielewa na wakakubali kubadilika.


“Mchezo wetu mbele ya Yanga niliwaambia vijana kwamba utakuwa mgumu na wa mbinu lazima tuwe makini. Kweli wachezaji wangu walipambana na tuliona ila mwisho kabisa dakika zile za lala salama tulifungwa.


“Kosa moja ambalo tulifanya tukasababisha kona ambayo iliwapa faida wapinzani wetu, hakuna namna lazima tuendelee kupambana kwa ajili ya mechi zinazokuja,” amesema.

Mchezo unaofuata kwa Mbeya City ni Septemba 20, itakuwa dhidi ya Azam FC, Uwanja wa Sokoine majira ya saa 8:00 mchana.

SOMA NA HII  KOCHA SIMBA: YANGA WAMESAJILI MAJEMBE