Home Uncategorized YANGA YAZIPIGIA HESABU POINTI TATU ZA COASTAL UNION

YANGA YAZIPIGIA HESABU POINTI TATU ZA COASTAL UNION


 KOCHA Msaidizi wa Yanga, Juma Mwambusi amesema kuwa ana imani kwamba wachezaji wake watakuwa kwenye ubora kwa kadri ambavyo wanaendelea kutimiza majukumu yao ndani ya uwanja pamoja na kucheza kwa kujituma.
 

Jana, Septemba 30 Yanga ilicheza mchezo wa kirafiki dhidi ya KMKM ya Zanzibar ambapo kwenye mchezo huo ilishinda kwa mabao 2-0 huku mtupiaji akiwa ni Tonombe Mukoko aliyetupia mabao hayo dakika ya 10 na dakika ya 30.


Oktoba 3, Yanga itakuwa na kibarua cha kumenyana na Coastal Union ya Tanga, Uwanja wa Mkapa mchezo unaotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kwa timu zote mbili kutokana na matokeo ya kwenye mechi zao za kwenye mzunguko wa nne.


Yanga ilikuwa ugenini ilishinda bao 1-0 mbele ya Mtibwa Sugar, Uwanja wa Jamhuri na Coastal Union ilikuwa nyumbani Uwanja wa Mkwakwani, Tanga na ilishinda kwa bao 1-0 mbele ya JKT Tanzania.


Akizungumza na Saleh Jembe, Mwambusi amesema kuwa wanaamini kwa maandalizi ambayo wanayafanya watapata matokeo chanya.


“Sio kazi nyepesi kupata ushindi ndani ya uwanja ila inahitaji maandalizi mazuri na makubwa. Tunachokifanya kwa sasa ni kuona tunakuwa na timu bora itakayotupa matokeo hivyo tutapambana mbele ya Coastal Union kupata ushindi.


“Timu nzuri ambayo tunakutana nayo hatuibezi tunawaheshimu wapinzani wetu lakini hamna namna tunahitaji ushindi na kupata pointi tatu, mashabiki wajitokeze kwa wingi,” amesema.

SOMA NA HII  LAMPARD ASHANGAZWA NA SILVA