Home Uncategorized SABABU YA SIMBA KUWAACHA BONGO NYOTA WAKE WATATU YAWEKWA WAZI

SABABU YA SIMBA KUWAACHA BONGO NYOTA WAKE WATATU YAWEKWA WAZI

 


BAADA ya Simba kuwaacha nyota wake watatu Chris Mugalu, Charles Ilanfya na David Kameta uongozi wa timu hiyo umefunguka juu ya sababu za kuwaacha nyota hao.

 

Simba jana Jumatano ilitia timu nchini Nigeria tayari kwa mchezo wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa dhidi ya Plateau FC ya nchini huko, mchezo ukitarajiwa kufanyika wikiendi hii.

  

Sven Vandenbroeck amesema kuwa majeruhi ya Mugalu na kutokuwa fiti kwa Ilanfya ni sababu ya kuwaacha nyota hao huku Kameta yeye akiachwa kutokana na kuwa katika majukumu ya timu ya taifa chini ya umri wa miaka 20, ambao wapo katika michuano ya CECAFA inayoendelea kufanyika mkoani Arusha.

 

“Wachezaji ambao wameachwa wote wana sababu zao mbalimbali na ukiziangalia ni za msingi katika mpira wa miguu na ndiyo maana umeona kuwa tumewaacha na si mambo mengine kama watu wengi ambavyo wanafikiria.

 

“Mugalu bado ni majeruhi na kwa Ilanfya yeye bado hayupo fiti hivyo hayupo tayari kwa mchezo huu na kuhusu Kameta yeye yupo katika majukumu ya timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 20, hivyo pia tusingeweza kuwa naye katika safari yetu,” amesema kocha huyo.

 

Mugalu ambaye alisajiliwa mwanzoni mwa msimu huu tayari ana mabao matatu kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu na anatajwa kuwa kati ya washambuliaji mahiri zaidi lakini akiwa anasumbuliwa na majeraha ya mara kwa mara.

SOMA NA HII  UNITED YASHINDA VITA YA KUMPATA NYOTA WA NIGERIA MBELE YA SPURS