Home Uncategorized YANGA: TUNAUTAKA UBINGWA WA LIGI KUU BARA

YANGA: TUNAUTAKA UBINGWA WA LIGI KUU BARA

 


KIUNGO wa Yanga, Feisal Salum Fei Toto’, amesema kuwa malengo yao wakiwa ni wachezaji msimu huu ni kuhakikisha wanaipatia ubingwa timu hiyo.

 

Yanga msimu huu imeanza ligi kwa kishindo ikiwa ni timu pekee ambayo haijapoteza mchezo hata mmoja kati ya michezo tisa waliyocheza ambapo wameshinda michezo saba na kutoa sare  mbili dhidi ya Tanzania Prisons na Gwambina FC.

 

Fei Toto amesema kuwa msimu huu malengo yao ni kuhakikisha wanaipatia Yanga ubingwa mara baada ya kukosa ubingwa huo kwa misimu mitatu, jambo ambalo wanaamini litakuwa zawadi kubwa kwa mashabiki wao.

 

“Tunafahamu kuwa mashabiki wa Yanga wana kiu kubwa ya ubingwa msimu huu na sisi wachezaji tumeweka malengo ya kuhakikisha tunatwaa ubingwa ili kuwapa zawadi hiyo na tutahakikisha tunaupambania ubingwa.

 

“Msimu huu ligi inaonekana kuwa ya ushindani kuliko msimu uliopita na hii ni kutokana na timu nyingi kujipanga kwa kufanya usajili makini, kwa kulitambua hilo ni lazima tuheshimu kila mchezo uliopo mbele yetu ili tupate pointi za kutufanya kuwa mabingwa,” amesema kiungo huyo.

 

Yanga, kwenye msimamo wa ligi wanashika nafasi ya kwanza wakiwa na pointi 23,  Azam FC ambao wapo nafasi ya pili wana pointi 22 na watani zao wa jadi Simba wapo nafasi ya tatu na pointi 19.


 

SOMA NA HII  GUARDIOLA:TULISTAHILI KUSHINDA ILA NDO HIVYO TENA