Home Uncategorized DALALI AKOMALIA JINA LAKE KUKATWA, AKIPEWA BARUA KUFANYA MAAMUZI

DALALI AKOMALIA JINA LAKE KUKATWA, AKIPEWA BARUA KUFANYA MAAMUZI


 MGOMBEA wa nafasi ya uenyekiti ndani ya Simba, Hassan Dalali ambaye jina lake limekatwa, amefunguka kuwa anasubiri akabidhiwe barua ndiyo achukue hatua.

 

Simba ipo katika mchakato wa kufanya uchaguzi mdogo kuziba nafasi ya mwenyekiti iliyoachwa na Swed Mkwabi.

 

Uchaguzi huo unatarajiwa kufanyika Februari 7,2021.Kamati ya Uchaguzi ya Klabu ya Simba, chini ya mwenyekiti wake, Boniface Lihamwike, imepitisha majina ya wagombea watano kati ya saba waliokuwa wakiwania nafasi hiyo baada ya kufanya usaili Desemba 27 na 28, mwaka huu.

 

Akizungumza na Spoti Xtra, Dalali alisema amesikia jina lake limekatwa kupitia vyombo vya habari na kuona katika mitandao ya kijamii, lakini bado hajakabidhiwa barua rasmi ya kuelezwa jambo hilo.

 

“Nimepata habari tu kupitia vyombo vya habari kuwa jina langu limekatwa lakini hadi sasa bado sijakabidhiwa barua, hivyo sitokuwa na nafasi nzuri ya kufanya maamuzi yoyote hadi nitakapopatiwa barua na kujua rasmi kama nimeondolewa.

 

“Bado kamati haijatupatia barua, kanuni zinasema majina yatabandikwa ndani ya saa 48 baada ya maamuzi, hivyo nasubiri nikishapata taarifa rasmi ndio nitajua nini cha kufanya kwani nitakuwa na uhakika kama nimekatwa au la,” alisema Dalali.

 

Waliopita kwenye uchaguzi huo ni Juma Nkamia, Murtaza Mangungu, Rashid Shangazi, Bittony Mwakisu na Hamis Omary. Walioenguliwa ni Hassan Dalali na Mohamed Soloka. 


Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Simba kwa majina yaliyotolewa ni ruksa kutoa pingamizi ambapo gharama ya kutoa pingamizi elfu thelathini na fedha za pingamizi ziwekwe kwenye akaunti ya Klabu ya Simba.

SOMA NA HII  MUONEKANO WA UKURASA WA MBELE GAZETI LA SPOTI XTRA ALHAMISI