Home Uncategorized SIMBA NA NAMUNGO WAMALIZA UTATA ISHU YA KICHUYA

SIMBA NA NAMUNGO WAMALIZA UTATA ISHU YA KICHUYA


BAADA ya winga Shiza Kichuya kucheza mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Azam Fc juzi Jumatatu akiwa na kikosi chake cha Namungo, wengi walishangazwa kutokana na taarifa zilizoenea mapema kwamba mchezaji huyo amefungiwa na FIFA.

Kichuya katika mchezo huo uliomalizika kwa sare ya bao 2-2 aliingia dakika 28 akichukua nafasi ya Abed Athuman na kucheza hadi dakika 90.

Awali, iliripotiwa kwamba mchezaji huyo atafungiwa kucheza soka kwa miezi sita baada ya klabu yake ya zamani, Pharco inayoshiriki Ligi Kuu nchini Misri kupeleka madai FIFA ya kuondoka huku akiwa ana mkataba nao.

Malalamiko hayo yamewafanya Simba kuingia katika matatizo ya kutakiwa kulipa fidia ya Sh 294 milioni ndani ya siku 45 kuanzia Novemba 24 mwaka huu hukumu ilipotolewa na FIFA kupitia Kamati ya Usuluhishi na migogoro.

Kocha Mkuu wa Namungo, Hemed, Morocco alisema alimtumia mchezaji huyo kwani hakuona kizingiti cha kumtumia.

“Hakuna barua ambayo imefika kwa viongozi wangu na ndio maana nimemtumia, mambo mengine ni viongozi watayaongelea hayo,” alisema kocha huyo.

Alipotafutwa msemaji wa Namungo, Kindamba Mila alisema hawajapokea barua rasmi iliyoonyesha Kichuya kufungiwa na ndio maana wameendelea kumtumia.

“Kuna email (barua pepe) ambazo zimeingia lakini sio za kufungiwa kwa Kichuya, ninachojua kama Simba watashindwa kulipa hiyo pesa ndipo Kichuya atafungiwa.”

Hata hivyo, habari za ndani ambazo Mwanaspoti ni kwamba Simba wameiomba FIFA adhabu hiyo kupitiwa upya.

Credit – Mwanaspoti

SOMA NA HII  KILICHO NYUMA YA MAFANIKIO YA KAGERA SUGAR HIKI HAPA