Home Burudani SERIKALI YAZUIA BASATA KUKAGUA NYIMBO ZA WASANII

SERIKALI YAZUIA BASATA KUKAGUA NYIMBO ZA WASANII


 SERIKALI imesitisha utekelezaji wa kanuni ya kukagua nyimbo za wasanii kabla hazijaenda kwa walaji.

 Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Innocent Bashungwa ametoa uamuzi huo Mei 8, 2021 alipokutana na viongozi wa mashirikisho kujadili kuhusu kanuni hiyo iliyoibua mijadala mingi mitandaoni.

 

Bashungwa amesitisha utekelezaji wa kanuni hiyo mpya ya kugagua nyimbo za wasanii kabla hazijaenda kwa walaji, iliyoanza kukaziwa utekelezaji wake Mei mwaka huu na Baraza la Sanaa la Taifa (Basata).

 

Baada ya kumalizika kwa kikao hicho kilichochukua takribani saa tatu, Waziri Bashungwa alieleza yaliyoafikiwa baada ya kupokea kwa maoni ya wadau na kueleza ameamua kusitisha utekelezaji wa kanuni hiyo.

 

“Baada ya kusitisha kanuni hii, kitakachofanyika ni Basata kukaa na wadau na kupokea maoni yao kuona namna gani bora ya kuja na kanuni za maadili ambazo hazitaumiza pande yoyote,” amesema Waziri Bashungwa.

 

Awali wasanii wakitoa maoni yao kuhusiana na kanuni hiyo,akiwemo Nikki Mbishi, amesema kanuni imetaja sanaa kwa ujumla, jambo ambalo litakuwa gumu katika utekelezaji.


“Sanaa ni uwanja mpana, kwa kanuni hii ni wazi kwamba hata nguo msanii atakayovaa inapaswa kwenda kukaguliwa kwanza na baraza kabla hajarekodi nyimbo au kupanda jukwaani,”.

 

Kwa upande wake Mwimbaji wa Taarabu, Mzee Yusufu ,amesema ipo haja ya Bongofleva kutengeneza kanuni zao kwa kuwa muziki wanaoufanya ni tofauti na ule wa dansi na taarabu.

 

Wakati Msanii Fid Q, amesema muziki kwa sasa ni biashara, hivyo unapouwekea mipaka ni kutaka kupoteza ubunifu na ushindani na wasanii wa ndani na nje ya nchi.

SOMA NA HII  MERIDIANBET SOKA BONANZA YAWA NURU KWA VIPAJI VYA VIJANA KIWALANI..