Home Ligi Kuu BIASHARA UNITED YAKOMALIA TANO BORA

BIASHARA UNITED YAKOMALIA TANO BORA


 UONGOZI wa Biashara United umeweka wazi kwamba hesabu zao ni kuona kwamba timu hiyo inamaliza ndani ya tano bora kwa msimu wa 2020/21.

Msimu huu Biashara United ni moja ya timu nne bora ndani ya ardhi ya Tanzania kwa kuwa imekuwa ikifanya vizuri kwenye mashindano yote ambayo inashiriki.

Katika Kombe la Shirikisho ilitinga hatua ya nusu fainali ambapo iliondolewa na Yanga kwa kufungwa bao 1-0 Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi.

Pia ndani ya ligi kwa sasa ipo nafasi ya nne ikiwa imekusanya jumla ya pointi 49 baada ya kucheza mechi 32.

Akizungumza na Saleh Jembe, Ofisa Habari wa Biashara United, Idrisa Sechombo amesema kuwa mipango inakwenda vizuri na wanahitaji kumaliza ndani ya tano bora.

“Kila kitu kinakwenda sawa kwa kuwa tunafanya vizuri katika mechi zetu tukiwa nyumbani hata ugenini kutokana na ubora wa kikosi hivyo tunaamini kwamba tutamaliza tukiwa ndani ya tano bora na nafasi hii ya nne ni muhimu kwetu.

“Kikubwa mashabiki wazidi kutupa sapoti kwa kuwa ushindani ni mkubwa ila wao tunawategemea pia katika kusaka mafanikio,” amesema.


Mechi mbili ambazo Biashara United imebakiwa nazo ndani ya ligi zote itakuwa ugenini ambapo moja kati ya hiyo ni dhidi Mbeya City ambayo inapambana kujinusuru kushuka daraja utapigwa Uwanja wa Sokoine.

SOMA NA HII  NAMUNGO: TUKO TAYARI KUUWASHA MOTO SHINYANGA