Home Makala SUALA LA UWANJA WA FAINALI YA FA ITAZAMWE KWA UMAKINI

SUALA LA UWANJA WA FAINALI YA FA ITAZAMWE KWA UMAKINI

 FAINALI ya Kombe la Shirikisho msimu huu inatarajiwa kuchezwa Uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma mchezo ambao unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kwa timu zote mbili ambazo zinahitaji ushindi.


Utakuwa ni mchezo mzuri kwa timu zote na imani yangu ni kuona kwamba kila timu iliyotinga fainali itafanya maandalizi mazuri.


Ikumbukwe kwamba Agosti 2 Uwanja wa Nelson Mandela, Sumbawanga fainali ilichezwa na Simba ilishinda mabao 2-0.


Ukweli ni kwamba waandaaji wa mashindano hayo wamekuja na kitu cha kipekee kuanzia ushindani ulivyo mwanzo pamoja na kila timu kupambana kufikia malengo ambayo wamejiwekea.


Katika hilo ninapenda kuwapa pongezi siku zote mashindano yamekuwa na mvuto wa kipekee huku kila timu ikiwa na nafasi ya kuibuka na ubingwa ikiwa itajipanga.


Ni timu nyingi ambazo zinakusanywa kwa kuwa inakusanya timu za madaraja yote kuanzia Ligi Daraja la Kwanza, Ligi Daraja la Pili mpaka Ligi Kuu Tanzania Bara.


Hapa nadhani unaona namna inavyokuwa na mvuto huku kila timu ikisaka ushindi kwenye mechi zake zote ili kufikia hatua ambayo wanahitaji.


Huku kila mchezo ni fainali kwani ukipigwa mchezo mmoja mwisho wa safari unawadia kwako na ndivyo ilivyokuwa kwa msimu huu wa mwaka 2020/21.


Yote kwa yote tumeshuhudia namna ilvyokuwa hatua kwa hatua mpaka kwenye hatua ile ambayo ilikuwa ina mvuto wa kipekee hatua ya robo fainali kisha nusu fainali na sasa ni fainali.


Zilizotinga fainali ni Simba na Yanga ambapo kwenye timu hizi mbili anakwenda kutafutwa bingwa wa Kombe la Shirikisho ambaye ataibuka kidedea tena nje ya Dar es Salaam.


Nina amini kuwa utakuwa mchezo mkubwa na wenye ushindani kwani kila timu inahitaji kupata ushindi ili kubeba taji kwani ndiyo malengo ya timu ambayo imetinga hatua ya fainali.


Sasa kinachonileta hapa leo nahitaji kuweka kwenye jamvi ni namna maandalizi yalivyo hasa kwenye fainali yenyewe inavyokuwa na inakokwenda kuchezwa.


Unajua kuna mambo mengine tunapaswa tutazame namna timu zinavyopambana kufikia mafanikio pamoja na kule ambako zinapelekwa kufanyia mashindano.


Haina maana kwamba Kigoma ni mbali ama hapafai hapana najua ni falsafa katika kuupeleka mpira kila kona ya Tanzania ila kuna mambo ya muhimu waandaaji wa mashindano haya wanapaswa wayatazame.


Unapoamua kupeleka fainali tena ya mashindano makubwa kama FA nje ya Dar es Salaam na kwenye mkoa ambao bado hakuna timu inayoshiriki Ligi Kuu Bara hii naona bado haijakaa sawa.


Msimu mmoja wakati nipo Lipuli nilifika na timu hatua ya fainali na ikachezwa huko Lindi, Ilulu haikuwa mbaya lakini ilikuwa na maumivu mengi.

SOMA NA HII  EDO KUMWEMBE : BWALYA ANAONDOKA LAKINI HATUNA MAJOZI NAYE....MISIMU YOTE HII ANA GOLI MBILI TU...


Achana na kupoteza kwa kufungwa bao 1-0 mbele ya Azam FC ninazungumzia mazingira ya Ilulu yalivyo hayakuwa rafiki kwa timu yangu pamoja na mimi kukaa huko hasa kwa upande wa maradhi na chakula.


Ilikuwa ni ngumu kwa timu kukaa sehemu moja kilichotakiwa kufanyika huko ni kuwagawa wachezaji kwa mafungumafungu ili waweze kukaa huko wakati wa maandalizi.


Pia upande wa miundombinu bado mambo mengi yanakuwa hayaleti picha nzuri zaidi ya kufanya mazingira kuwa magumu kwa wachezaji wote.


Tazama namna ambavyo gharama zilitumika kukikarabati kiwanja cha Ilulu kwa ajili ya fainali ya siku moja nini kimetokea kwa sasa? Hakuna timu ambayo inatumia kiwanja kile baada ya fainali.


Msimu uliopita ilikuwa ni Uwanja wa Nelson Mandela, angalua ninaona kwamba ule uwanja unatunzwa hasa baada ya Tanzania Prisons kuamua kuutumia uwanja ule.


Itapendeza ikiwa waandaaji wataamua kuweka usawa katika maandalizi ya fainali ya Kombe la Shirikisho hasa kwa kuwa na sehemu moja ambayo itakuwa inajulikana na kila mchezaji tangu mwanzo wa mashindano.


Unajua haya mashindano yana hadhi ya kimataifa na mshindi pia anapata nafasi ya kushiriki michuano mikubwa ya kimataifa hivyo itapendeza maboresho katika sehemu ya kuchezea fainali.


Bado nina amini kuwa Kigoma kutakuwa na tatizo la malazi kwa timu pamoja na viongozi hivyo mazingira yanaweza kuwa sawa na kule Ilulu ama ilivyokuwa Subawanga  hivyo ni muhimu kutazama upya katika kuandaa uwanja wa kuchezea fainali.


Sikatai kucheza Sumbawanga, ama Kigoma  hata ingepelekwa Njombe sawa hakuna tatizo lakini cha msingi ni kuangalia hadhi ya mashindano pamoja na gharama za maandalizi ya uwanja kwa wakati mmoja.


Labda kwa mfano tuseme  gharama za maboresho ya uwanja zingepelekwa pale Tanga Mkwakwani huenda ingepunguza kelele kwamba Mkwakwani hakuna uwanja mzuri.


Na ingesaidia pia kuongeza idadi ya viwanja bora ndani ya ligi msimu ujao kwa kuwa kuna timu za Ligi Daraja la Kwanza pamoja na Ligi Kuu zingeendelea kuutumia uwanja huo.


Ninadhani ingependeza tukifuata mfano wa FA ya Ulaya kule wenzentu wanachezea fainali pale Wembeley pana faida na ushindani unakuwa mkubwa huku wachezaji wakiweka alama kwamba wamewahi kucheza ndani ya uwanja mzuri duniani.


Kwa Tanzania ingekuwa inachezwa pale Uwanja wa Taifa ingependeza zaidi na kila mchezaji angekuwa anatambua kwamba anakwenda kucheza Uwanja wa Taifa.


Ujue kucheza Uwanja wa Taifa ni CV kuna wachezaji wengine wanaskia tu hawajawahi kucheza pale, nina amini kwamba katika hili wakati ujao itafanyiwa maboresho.

Anaandika Seleman Matola, kupitia Championi